MAHAKAMA KUAMUA KESI YA DIKTETA UCHWARA NOVEMBA 16 MWAKA 2017

Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu inatarajia kutoa uamuzi dhidi ya Mbunge wa Singida Mashariki, Tundu Lissu (Chadema), kama ana kesi ya kujibu ama la katika kesi ya ‘Dikteta Uchwara’ Novemba 16, mwaka huu.


Mahakama hiyo mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Godfrey Mwambapa, ilitoa uamuzi jana baada ya Jamhuri kufunga ushahidi ukiwa na mashahidi watano.


Wakili wa Serikali, Hamis Said, alidai kesi ilikuja kwa ajili ya uamuzi wa mahakama na kwamba mshtakiwa anaumwa amelazwa katika Hospitali ya Chandaria Accident and Emergence iliyopo Nairobi.


Wakili wa utetezi, Peter Kibatala, alidai anatarajia kuwasilisha hoja za maandishi ili kuishawishi mahakama kuwa mteja wake hana kesi ya kujibu Oktoba 9, 2017.


Lissu anakabiliwa na mashtaka ya kutoa kauli za uchochezi dhidi ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano.


Juni 30, mwaka 2016, Lissu alifikishwa mahakamani hapo kwa mara ya kwanza na kufunguliwa kesi ya uchochezi namba 233/2016, ambapo alisomewa shtaka la kutoa maneno ya uchochezi nje ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu Juni 28, mwaka huo, kwa kumuita Rais wa nchi ni dikteta uchwara, kinyume cha kifungu namba 32 cha Sheria ya Magazeti ya Mwaka 1976.


Anadaiwa katika viwanja vya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, alitoa kauli za uchochezi kwamba ‘Mamlaka ya Serikali mbovu ni ya kidiktekta uchwara, inahitaji kupingwa na kila Mtanzania kwa nguvu zote, huyu diktekta uchwara lazima apingwe kila sehemu. Kama uongozi utafanywa na utawala wa kijinga nchi inaingia ndani ya giza nene’.


Jamhuri katika kesi hiyo iliita mashahidi watano, akiwamo Mrakibu Msaidizi wa Polisi (ASP) Kimweli na Staff Sajenti Ndege.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments