MBUNGE MCHUNGAJI MSIGWA ASHUSHWA JUKWAANI KISHA KUKAMATWA NA POLISI

Mbunge wa Iringa Mjini Peter Msigwa (Chadema) amekamatwa na polisi leo Jumapili jioni baada ya kushushwa jukwaani kwenye mkutano wa hadhara katika Kata ya Mlandege mkoani Iringa.


Mwenyekiti wa Baraza la Vijana wa Chadema Iringa Mjini (Bavicha), Leonce Marto amesema kuwa mbunge huyo alikamatwa saa 11:24 jioni na Mkuu wa Upelelezi wa Mkoa (RCO) aliyekuwa ameambatana na polisi wengine kisha wakampeleka ofisi za mkoa za jeshi hilo.


“Kutoka Mlandege mpaka ofisini kwa kamanda wa mkoa amebadilishwa kwenye magari matatu. Tunahisi atakuwa anasafirishwa ingawa bado anahojiwa. Yupo ndani, sisi tunaendelea kumsubiri nje,” amesema Marto.


Mwenyekiti huyo alibainiha kwamba mpaka wakati huo (saa 12:30 jioni) jeshi hilo halikubainisha sababu za kumshikilia Msigwa.


“Alikuwa na kibali cha kufanya mkutano katika kata tatu kuanzia leo Jumapili mpaka Jumanne. Alianza kuzungumza saa tisa alasiri ilipofika saa 11:24 jioni, RCO akiwa na polisi wengi wakamshusha jukwaani na kuondoka naye,” alisema Marto bila kufafanua sababu za kukamatwa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527