KATIBU MTENDAJI BODI YA FILAMU AWATAKA WATANZANIA KUJIANDAA TAMASHA LA JAMAFEST


Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu nchini Tanzania Bi.Joyce Fisso amewataka watanzania kujiandaa na kutumia vyema fursa ya kuwa wenyeji wa Tamasha la Utamaduni na Sanaa Afrika Mashariki (JAMAFEST) litakalofanyika nchini mwaka 2019.

Akizungumza na BMG leo, Bi.Fissoo ambaye pia alikuwa Mjumbe wa Kamati ya Maandalizi ya Tamasha la JAMAFEST 2017 lililomalizika Kampala nchini Uganda, amesema tamasha hilo linatoa fursa kubwa kwa watanzania kuonyesha ngoma na bidhaa mbalimbali za kiutamaduni na hivyo kukuza soko lao la ndani na nje ya nchi.

Aidha Bi.Fissoo amefurahishwa kwa namna watanzania walivyoshiriki vyema kwenye tamasha la mwaka huu nchini Uganda na kubainisha kwamba walitia fora kwenye maonyesho ya tamasha hilo yaliyofanyika kwenye viwanja vya Kokolo.

Katika kilele cha Tamasha la Utamaduni na Sanaa Afrika Mashariki JAMAFEST mwaka 2017 nchini Uganda, Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo wa Tanzania, Mhe.Dkt.Harrison Mwakyembe alipokea bendera ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kama ishara ya Tanzania kuwa mwenyeji wa tamasha hilo ambalo kwa mara ya kwanza liliasisiwa nchini Rwanda mwaka 2013.
Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu nchini Tanzania ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati ya Maandalizi Tamasha la JAMAFEST Bi.Joyce Fisso (mwenye bendera) akijiandaa kupokea cheti cha pongezi kutoka kwa Waziri wa Wizara ya Afrika Mashariki ya Uganda Mhe.Ali Kivejinja kwenye kilele cha Tamasha la Utamaduni na Sanaa Afrika Mashariki JAMAFEST lililofanyika Kampala nchini Uganda Septemba 14,2017.
Naibu Balozi wa Tanzania nchini Uganda, Balozi Elibariki Maleko (wa pili kulia) akipokea cheti cha pongezi kutoka kwa Katibu Mtendaji wa Bodi ya Filamu Bi.Joyce Fissoo kwenye kilele cha Tamasha la JAMAFEST ambapo Tanzania ilishiriki vyema kwenye tamasha hilo lililofikia tamati Septemba 14,2017 nchini Uganda.
Waziri wa Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo nchini, Mhe.Dkt.Harrison Mwakyembe alipokea bendera ya Jumuiya ya Afrika Mashariki kama ishara ya Tanzania kuwa mwenyeji wa Tamasha la Utamaduni na Sanaa Afrika Mashariki JAMAFEST mwaka 2019 ambapo kwa mara ya kwanza tamasha hilo liliasisiwa mwaka 2013 nchini Rwanda. Picha kwa hisani ya Binagi Media Group

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527