JAJI MKUU WA TANZANIA AMPONGEZA JAJI MKUU WA KENYA KWA UJASIRI WAKE WA KULINDA UHURU WA MAHAKAMA

Jaji Mkuu wa Kenya, David Maraga ametua nchini katika mkutano wa majaji na mahakimu akionekana kivutio kwa wengine.


Jaji huyo ni mmoja wa majaji wakuu 13 kutoka nchi mbalimbali duniani wanaohudhuria mkutano majaji na mahakimu wa nchi za Jumuiya ya Madola unaofanyika jijini Dar es Salaam kwa siku tatu..


Maraga amegeuka kivutio baada ya kushangiliwa na majaji waliohudhuria mkutano huo wakati alipotambulishwa na Jaji Mkuu wa Tanzania, Profesa Ibrahim Juma.


Profesa Juma amempongeza Maraga kwa kuwakilisha mfano bora wa kulinda uhuru wa Mahakama kwa nchi nyingine duniani.


Kiongozi huyo ameonekana akiwa ameambatana na walinzi wanne ambao wanamfuata popote anapotembea nje ya mkutano huo.


Hata hivyo, Maraga amekataa kuzungumza na vyombo vya habari kwa madai amekuja kuhudhuria mkutano huo na siyo kwa jambo jingine lolote.


Mkutano huo umefunguliwa leo Jumatatu na Makamu wa Rais, Samia Suluhu ukiwa na kauli mbiu "Kujenga Mahakama Shirikishi, Thabiti na Inayowajibika."


Jaji Maraga kwa siku za hivi karibuni amekuwa maarufu baada ya kutoa uamuzi wa kufuta Uchaguzi Mkuu wa Kenya uliokuwa umempa ushindi Rais Uhuru Kenyatta.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527