Picha: MGODI WA BULYANHULU WAKABIDHI JENGO LA MADARASA NA VITANDA VYA WAGONJWA HALMASHAURI YA MSALALA KAHAMA

Muonekano wa jengo la madarasa mawili lililojengwa na mgodi wa Acacia Bulyanhulu katika shule ya msingi Lwabaganga katika halmashauri ya Msalala wilayani Kahama mkoa wa Shinyanga.
Moja ya vitanda viwili vya kisasa kwa ajili ya wagonjwa kilichotolewa na mgodi wa Bulyanhulu katika kituo cha afya Bugarama halmashauri ya Msalala-Picha na Kadama Malunde -Malunde1 blog

****


Mgodi wa dhahabu wa Bulyanhulu umekabidhi rasmi jengo jipya la madarasa mawili yaliyojengwa na mgodi huo katika shule ya msingi ya Lwabakanga iliyopo katika kijiji cha Lwabakanga kata ya Bulyanhulu halmashauri ya Msalala wilaya ya Kahama mkoa wa Shinyanga ambayo wanafunzi wake walikuwa wanasomea chini ya mti.

Mgodi huo pia umekabidhi vitanda viwili vya kisasa vya kutolea huduma katika kituo cha afya Bugarama kilichopo katika kijiji cha Bugarama kata ya Bugarama katika halmashauri ya Msalala ambavyo vitasaidia madaktari na wauguzi kutoa huduma bora kwa wagonjwa.

Mgeni rasmi wakati wa makabidhiano hayo ya jengo la madarasa na vitanda vya wagonjwa yaliyofanyika leo Ijumaa Agosti 18, 2017 alikuwa kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya Msalala Julius Buberwa.

Akizungumza wakati wa kukabidhi jengo jipya la madarasa katika shule ya msingi Lwabakanga,Kaimu Meneja wa mgodi wa Bulyanhulu,Bryson Tarimo alisema mradi huo wa madarasa mawili ni sehemu ya uwajibikaji wa kampuni kwenye jamii ambapo Mgodi umetumia shilingi milioni 95 (95,365,000/=) ambayo yatachangia kuongeza idadi ya madarasa katika shule hiyo mpya yenye wanafunzi 483.

“Tunaamini kuwa elimu ni nguzo muhimu ya maendeleo ya nchi na duniani kwa ujumla na ndiyo maana mgodi hadi sasa umeshiriki kuchangia kwa namna mbalimbali ujenzi wa madarasa 35 katika shule za jirani na mgodi kwa miaka iliyopita”,alieleza Tarimo.

Alizitaja baadhi ya shule za halmashauri ya Msalala ambazo Mgodi wa Bulyanhulu umewahi kutoa usaidizi kwenye miradi ya kuboresha elimu katika maeneo mbalimbali ikiwemo ujenzi wa shule,maabara za sayansi,nyumba za walimu,madarasa,vyoo,umeme na maji,fensi na vifaa vya ujenzi kuwa ni shule za Msingi Kakola A, Kakola B, Kakola C, Nyangaka, Bugarama, Busindi, Buyange, Ibanza, Igwamanoni, Lwabakanga,shule za sekondari ri Bugarama, Bulyanhulu na Nyikoboko.

Alisema mbali na kutoa usaidizi katika shule za Msalala pia mgodi huo umesaidia shule zilizopo halmashauri ya wilaya ya Nyang’wale mkoani Geita ambazo ni shule za msingi Hussein Nassor iliyojengewa madarasa, vyoo na nyumba za walimu na Mwingiro iliyopewa madawati pamoja na shule ya sekondari Nyijundu iliyojengewa maabara za Sayansi na mfumo wa kuvuna maji ya mvua.

Akikabidhi vitanda vya kisasa katika kituo cha afya Bugarama,Tarimo alisema vitanda hivyo vitasaidia madaktari na wauguzi kutoa huduma bora kwa wagonjwa na kurahisisha huduma kwa wananchi ili kuhakikisha huduma za afya zinakuwa bora zaidi.

“Kama ilivyo katika sehemu mbalimbali duniani pia hapa nchini Tanzania watu wengi hawana huduma za afya karibu na makazi yao hasa maeneo ya vijijini, katika kipindi cha miaka michache iliyopita mgodi wetu umefanya kazi na halmshauri ya Msalala na wadau wengine wa sekta ya afya kutekeleza baadhi ya miradi ya kuboresha huduma za afya kwa ujumla ndani ya mkoa wa Shinyanga lakini pia mkoa wa Geita”,alieleza Tarimo.

Alisema mgodi huo umekuwa na utamaduni wa kusaidia jamii katika sekta ya afya kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita mgodi umetoa misaada mbalimbali ikiwemo ujenzi wa kituo cha afya Bugarama ,Zahanati ya Kakola, Kisima cha maji Kabale kwa zahanati ya Kakola,mradi wa Umeme kwa ajili ya zahanati ya kijiji cha Kakola na Msaada wa vifaa tiba mbalimbali katika kituo cha Bugarama katika halmashauri ya Msalala.

Pia tumesaidia ujenzi wa wodi ya wajawazito katika hospitali ya wilaya ya Kahama, msaada wa Machine ya Incubator kwa ajili ya wodi ya wajawazito hospitali ya mkoa wa Shinyanga, na kwa Wilaya ya Nyang’hwale tumetoa kitanda cha kufanyia upasuaji kwa ajili ya kituo cha afya cha wilaya,Misaada ya vifaa tiba mbalimbali katika kituo cha afya Kharumwa na msaada wa vifaa tiba kwa wajawazito zahanati ya Mwingiro”,alieleza Tarimo.

Akipokea jengo la madarasa mawili na vitanda viwili vya kutolea huduma za afya,Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya Msalala,Julius Buberwa aliushukuru mgodi huo kwa misaada na huduma ambazo mgodi umekuwa ukitoa kwa jamii na kuwaomba waendelee kusaidia kwa bado jamii ina mahitaji mengi.

“Niwashukuru sana kwa kujenga madarasa katika shule ya Msingi Lwabaganga ambayo wanafunzi wake walikuwa wanasomea nje chini ya mti,naamini sasa wanafunzi waliopo hapa sasa watatumia madarasa haya,lakini pia ndugu zetu madaktari na wauguzi mmewarahisishia kazi ya utoaji huduma za afya kwa wagonjwa kwa kuwapatika vitanda hivi vya kisasa kabisa ambavyo vitatumika katika chumba cha wagonjwa mahututi”,aliongeza Mkurugenzi.

NIMEKUWEKEA HAPA PICHA ZA MATUKIO WAKATI WA MAKABIDHIANO YA JENGO LA MADARASA KATIKA SHULE YA MSINGI LWABAKANGA NA VITANDA VYA VIWILI VYA KISASA KATIKA KITUO CHA AFYA BUGARAMA

Muonekano wa jengo la madarasa mawili lililojengwa na mgodi wa Acacia Bulyanhulu katika shule ya msingi Lwabaganga katika halmashauri ya Msalala wilayani Kahama mkoa wa Shinyanga.-Picha zote na Kadama Malunde-Malunde1 blog

Kaimu Meneja wa mgodi wa Bulyanhulu,Bryson Tarimo akizungumza wakati wa kukabidhi jengo la madarasa mawili katika shule ya msingi Lwabakanga iliyopo katika kata ya Bulyanhulu halmashauri ya Msalala wilaya ya Kahama.

Kaimu Meneja wa mgodi wa Bulyanhulu,Bryson Tarimo akielezea namna mgodi huo uliguswa na mazingira magumu waliyokuwa wanasomea wanafunzi wa shule hiyo changa ambayo hivi sasa ina wanafunzi kuanzia darasa la awali hadi darasa la tatu ambao walikuwa wanasomea chini ya mti.

Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya Msalala,Julius Buberwa akizungumza wakati mgodi wa Bulyanhulu ukikabidhi jengo la madarasa katika ya msingi Lwabakanga.Kulia ni kaimu Afisa elimu kata ya Bulyanhulu,Joyce Lwanji na mwalimu mkuu wa shule ya msingi Lwabakanga,Joseph Mgote.

Kulia ni Mtaalamu wa Mawasiliano Mgodi wa dhahabu wa Acacia Bulyanhulu Mary Lupamba,Mkuu wa kitengo cha Mahusiano ya jamii mgodi wa Bulyanhulu ,Sara Ezra Teri na Kaimu Meneja wa mgodi wa Bulyanhulu,Bryson Tarimo na Kaimu Meneja wa mgodi wa Bulyanhulu,Bryson Tarimo,wengine ni wafanyakazi wa halmashauri ya Msalala.

Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya Msalala,Julius Buberwa akizungumza katika eneo ambalo lilikuwa linatumika kama darasa kwa ajili ya wanafunzi wa darasa la tatu katika shule ya msingi Lwabakanga.

Mkuu wa kitengo cha Mahusiano ya jamii,Sara Ezra Teri akisitiza jambo wakati wa makabidhiano ya jengo la madarasa.Kulia ni Mtaalamu wa Mawasiliano Mgodi wa dhahabu wa Acacia Bulyanhulu Mary Lupamba.

Mkuu wa kitengo cha Mahusiano ya jamii,Sara Ezra Teri akielezea namna mgodi huo unavyosaidia katika sekta ya elimu kwa wananchi wanaozungumza mgodi huo.

Mtaalamu wa Mawasiliano Mgodi wa dhahabu wa Acacia Bulyanhulu Mary Lupamba akisisitiza jambo.

Mgeni rasmi na viongozi kutoka mgodi wa Acacia Bulyanhulu katika shule ya msingi Lwabaganga wakielekea katika jengo hilo kwa ajili ya makabidhiano.

Kaimu Meneja wa mgodi wa Bulyanhulu,Bryson Tarimo akikabidhi funguo za jengo hilo kaimu mkurugenzi wa halmashauri ya Msalala,Julius Buberwa.

Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya Msalala,Julius Buberwa akifungua mlango wa moja ya madarasa katika jengo hilo.

Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya Msalala,Julius Buberwa kaimu afisa elimu wa kata ya Bulyanhulu,Joyce Lwanji wakisaini hati ya makabidhiano.

Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya Msalala,Julius Buberwa kaimu afisa elimu wa kata ya Bulyanhulu,Joyce Lwanji wakionesha hati ya makabidhiano ya jengo hilo.

Wanafunzi wa darasa la tatu wakiwa katika darasa jipya badala ya lile la chini ya mti.

Wanafunzi wa shule ya msingi Lwabakanga wakiwa katika darasa lao la chini ya mti.

Awali wanafunzi wa darasa la tatu katika shule ya msingi Lwabakanga wakiwa katika darasa lao la chini ya mti.

Mwalimu Matendo Yusuph akiwa na wanafunzi wake chini ya mti.

Moja kati ya vyoo vilivyopo katika shule ya msingi Lwabakanga vilivyojengwa na mgodi wa Bulyanhulu ambavyo vilikabidhiwa hivi karibuni baada ya ujenzi kukamilika.
Picha ya pamoja katika jengo jipya la madarasa mawili lililojengwa na mgodi wa Bulyanhulu.
Hapa ni katika kituo cha afya Bugarama: Pichani ni Moja kati ya vitanda viwili vya kisasa kwa ajili ya kutolea huduma za afya katika kituo cha afya Bugarama katika halmashauri ya Msalala vilivyotolewa na mgodi wa Bulyanhulu.

Kaimu Meneja wa mgodi wa Bulyanhulu,Bryson Tarimo akiangalia kitanda kabla ya kukabidhi kwa Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya Msalala,Julius Buberwa.

Kaimu Meneja wa mgodi wa Bulyanhulu,Bryson Tarimo akikabidhi vitanda kwa Kaimu Mkurugenzi wa halmashauri ya Msalala,Julius Buberwa.
 Kaimu Mganga mkuu wa halmashauri ya Msalala,Flora Magembe akizungumza wakati wa makabidhiano hayo ambapo aliushukuru mgodi wa Bulyanhulu kwa kuendelea kusaidia jamii katika sekta ya afya.
Mganga mkuu wa kituo cha afya Bugarama,Dk. Emmanuel Joseph akielezea namna vitanda hivyo vinavyofanya kazi kwa kutumia remote na kwamba watavitumia zaidi katika chumba cha wagonjwa mahututi.

Picha ya pamoja baada ya makabidhiano ya vitanda.

Mganga mkuu wa kituo cha afya Bugarama,Dk. Emmanuel Joseph akisukuma kitanda kuelekea kwenye chumba cha wagonjwa mahututi.

Picha zote na Kadama Malunde-Malunde1 blog

SOMA HAPA CHINI TAARIFA ZA HUDUMA ZA AFYA NA ELIMU ZINAZOTOLEWA NA MGODI WA BULYANHULU- KUNA KIINGEREZA NA KISWAHILI↧↧



Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527