MADIWANI DODOMA WAMNG'OA MEYA...HAWANA IMANI NAYE


Jafari Mwanyemba
***
MADIWANI wa Manispaa ya Dodoma wamemwondoa Meya wao, Jafari Mwanyemba kwa kumpigia kura ya kutokuwa na imani naye kutokana na kumtuhumu kuhusika na tuhuma mbalimbali zikiwamo za ubadhirifu wa fedha.

Kura hizo zilipigwa mjini hapa kwenye Mkutano Maalumu wa Madiwani wa kujadili tuhuma dhidi ya Meya Mwanyemba.

Kati ya madiwani wa manispaa hiyo 56, 47 ndio walipiga kura ya kutokuwa na imani naye dhidi ya kura nne zilizodai kuwa na imani naye, wakati kura moja iliharibika na madiwani wanane hawakupiga kura.

Akitangaza matokeo hayo, Mkurugenzi Mtendaji wa Manispaa, Godwin Kunambi alisema kuanzia saa 8.30 adhuhuri hiyo, Mwanyemba si Meya wa Manispaa ya Dodoma na kutokana na kanuni za manispaa, Naibu Meya Jumanne Ngede ndiye atakayekuwa akiongoza hadi uchaguzi wa kuziba nafasi utakapofanyika miezi miwili kuanzia sasa.

Alisema kutokana na kanuni za halmashauri hiyo namba 4 (8), baada ya Tume iliyoundwa na Mkuu wa Mkoa kurudisha ripoti kwa mkurugenzi katika kipindi cha siku 14, alitakiwa kuwasilisha kwenye mkutano maalumu wa madiwani kwa uamuzi wa tuhuma dhidi ya meya huyo ambapo madiwani wameamua kumng’oa kwa kupigia kura.

Kutokana na kupigwa kura ya kumng’oa, kanuni za halmashauri zinamruhusu aliyekuwa Meya wa Manispaa ndani ya mwezi mmoja kukata rufaa kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527