Picha 10: DC SHINYANGA AFUNGUA MAFUNZO USAJILI WA WATOTO KUPATA VYETI VYA KUZALIWA



Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro leo Jumatano Machi 15,2017 amefungua mafunzo ya siku tatu kuhusu usajili wa watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga.

Mafunzo hayo yanahudhuriwa na maafisa watendaji wa kata 26 pamoja na wasaidizi wao na watoa huduma katika vituo vya afya na zanahati zilizopo katika halmashauri hiyo.

Mafunzo hayo yameandaliwa na Wakala wa Usajili wa Vizazi na Vifo nchini RITA kwa ufadhili wa shirika la watoto la UNICEF.

Akizungumza wakati wa kufungua semina hiyo Matiro alisema kuanzia sasa vyeti vya kuzaliwa vya watoto vitatolewa katika ofisi ya mkurugenzi wa halmashauri badala ya ofisi ya mkuu wa wilaya ili kuwarahisishia wananchi kupata huduma hiyo.

“Zoezi la kusajili watoto sasa linakabidhiwa kwenye ofisi ya mkurugenzi wa halmashauri na taarifa za watoto zitaanza kuchukuliwa katika ofisi za kata na vituo vya afya na zahanati ambapo maafisa watendaji na watoa huduma watawajibika kuwatafuta watoto walio chini ya miaka mitano ili wapatiwe vyeti vya kuzaliwa bure”,alieleza Matiro. 

Mkuu huyo wa wilaya alisema zoezi la kutoa huduma ya usajili kuanzia ngazi ya kata litapunguza msongamano katika ofisi ya mkuu wa wilaya ambapo wananchi walikuwa wanatumia muda mwingi na kusafiri umbali mrefu kutoka vijijini kutafuta huduma ya kusajili watoto wao.

Naye Ofisa usajili kutoka makao makuu (Rita ) Emiliana Mmbando alisema zoezi la kusajili limeanza kufanyika katika mkoa wa Shinyanga na Geita na kuongeza kuwa changamoto iliyopo ni wazazi wengi kutokuwa na uelewa kuhusu vyeti na wengi wakilalamikia umbali wa kufuatilia vyeti hivyo.

Alisema zoezi la kusajili watoto litaanza rasmi tarehe 21,mwezi Machi mwaka 2017.

Tazama picha matukio wakati wa semina hiyo ya siku tatu iliyoanza Machi 15,2017.
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza katika semina kuhusu usajili wa watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano katika ukumbi wa vijana Center uliopo katika kanisa la Mama Mwenye Huruma Ngokolo Mjini Shinyanga leo Jumatano Machi 15,2017-Picha zote na Kadama Malunde-Malunde1 blog
Washiriki wa semina hiyo wakiwemo maafisa watendaji wa kata na watoa huduma za afya katika vituo vya afya na zahanati katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza ukumbini ambapo mbali na kuwahamasisha kuandikisha watoto pia aliwataka maafisa watendaji wa kata kuhakikisha kuwa watoto wote wanaotakiwa kuandikishwa shuleni waandikishwe
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza na washiriki wa semina hiyo 
Mkuu wa wilaya ya Shinyanga Josephine Matiro akizungumza ukumbini.Kulia ni Afisa Maendeleo halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Daudi Kisangure,kushoto kaimu mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Julius Mlongo
Afisa Maendeleo halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Daudi Kisangure akizungumza wakati wa semina hiyo ambapo alisema
Wawezeshaji wakiwa ukumbini
Kaimu mkurugenzi wa halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Julius Mlongo
Afisa wa usajili kutoka RITA ,Emiliana Mmbando akizungumza ukumbini ambapo alisema zoezi la kuandikisha watoto linaloanza Machi 21,2017 litatolewa bure na vyeti vitatolewa bure kwa watoto wenye umri chini ya miaka mitano
Mwenyekiti wa maafisa watendaji katika halmashauri ya wilaya ya Shinyanga Emmanuel Maduhu akizungumza kwenye semina hiyo.

Picha zote na Kadama Malunde-Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527