Picha: MBUNGE WA JIMBO LA SHINYANGA MJINI STEPHEN MASELE AMALIZA ZIARA JIMBONI,WANANCHI WALIA NJAA


Mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini mheshimiwa Stephen Masele kupitia Chama Cha Mapinduzi (CCM) amemaliza kufanya ziara yake ya siku tatu katika jimbo la Shinyanga mjini.



Katika ziara hiyo ya kikazi iliyoanza Februari 15,2017 kumalizika Februari 17,2017 ,Mheshimiwa Masele amekagua miradi ya maendeleo na kufanya vikao na wananchi wa kata 14 kisha kujadili na kuzitafutia ufumbuzi kero za wananchi.

Katika maeneo mengi aliyopita,Mheshimiwa Masele amekutana na kilio kikubwa cha tatizo la njaa linalowakabili wananchi ambao walidai wamekuwa wakiendesha maisha yao kwa kunywa uji hivyo kuiomba serikali iwaone kwa jicho la huruma na kuwapatia chakula.

Mheshimiwa Masele pia amekumbana na kilio cha bei kubwa ya maji inayotozwa na Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira katika manispaa ya Shinyanga (SHUWASA),huku wananchi katika maeneo ambayo hayajafikiwa na mtandao wa maji kutoka ziwa Victoria wakiomba huduma hiyo ili kuondokana na kero ya maji.

Viongozi wa shule za msingi nao walipaza sauti zao juu ya uhaba wa walimu katika shule,matundu machache ya vyoo ukilinganisha na idadi kubwa ya wanafunzi,upungufu wa madarasa huku wengine wakiomba kupatiwa huduma ya maji na umeme katika shule zao.

Akizungumza wakati wa ziara hiyo,Mheshimiwa Masele alisema yeye kama mbunge hayupo tayari kunyamaza juu ya matatizo yanayowakabili wananchi wake na kuahidi kuendelea kushirikiana na mamlaka zinazohusika ili kumaliza changamoto hizo.

“Naomba serikali yetu itambue kuwa wananchi wa jimbo la Shinyanga Mjini wana njaa,wanahitaji chakula,hatuhitaji chakula cha bure bali tunataka chakula cha bei nafuu,wananchi wanalala njaa,shule zetu hazina walimu wa kutosha,bado bei ya maji iko juu sana ukilinganisha na kipato cha wananchi”,alieleza Masele.

Siku ya kwanza ya ziara,mheshimiwa Masele alitembelea mradi mkubwa wa ujenzi wa daraja la Galamba na kuangalia,siku ya pili na tatu katika ziara yake ametembelea shule za msingi na kufanya vikao mbalimbali.

Mwandishi mkuu wa Malunde1 blog,Kadama Malunde,alikuwepo kwenye ziara hiyo…Ametuletea Picha 53 za Matukio yaliyojiri siku ya pili na ya tatu ya Ziara ya Mheshimiwa Stephen Masele…Tazama hapo chini

SIKU YA PILI ZIARA YA MBUNGE WA JIMBO LA SHINYANGA MJINI MHESHIMIWA STEPHEN MASELE
Hapa ni katika Shule ya Msingi Twende Pamoja iliyopo katika kijiji cha Mwamalili kata ya Mwamalili katika Manispaa ya Shinyanga.Katikati ni Mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini mheshimiwa Stephen Masele (CCM) akienda kuangalia eneo ambapo patajengwa choo kwa ajili ya wanafunzi wa shule hiyo.Kulia ni diwani wa kata ya Mwamalili Paul Machela (CCM),wa kwanza kushoto 
Mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini mheshimiwa Stephen Masele akiangalia eneo ambapo patajengwa choo kwa ajili ya shule ya msingi Twendepamoja yenye jumla ya wanafunzi 820 wanaotumia matundu 6 ya choo na walimu 8 pekee.Wa kwanza kushoto ni mwalimu Cephrine Philip anayefundisha katika shule hiyo.
Mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini mheshimiwa Stephen Masele akiwasalimia wanafunzi wa shule ya msingi Twende Pamoja ambapo alisema kupitia mfuko wa jimbo ametoa shilingi milioni mbili kwa ajili ya kusaidia ujenzi wa shule hiyo.
Hapa ni katika shule ya Msingi Ujamaa katika kijiji cha Seseko kata ya Mwamalili.Kulia ni Mwalimu mkuu Msaidizi katika shule hiyo Regina Bundala akimwonesha mheshimiwa Masele eneo ambapo watajenga choo kipya kwa ajili ya shule hiyo yenye wanafunzi 662 wakitumia matundu manne ya choo huku walimu nane waliopo katika choo hicho wakiwa hawana choo.
Katikati ni Mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini mheshimiwa Stephen Masele akizungumza akiwa katika ofisi ya walimu shule ya msingi Ujamaa ambapo alisema mfuko wa jimbo umetoa shilingi milioni 2 kwa ajili ya ujenzi wa choo cha wanafunzi na walimu wa shule hiyo.Kulia ni Kaimu Afisa Elimu wa manispaa ya Shinyanga Gideon Kyungai,kushoto ni diwani wa kata ya Mwamalili Paul Machela.
Mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini mheshimiwa Stephen Masele akiwasalimia wanafunzi wa shule ya msingi Ujamaa na kuwataka wasome kwa bidii kwani elimu ina faida na itawasaidia kujikomboa katika maisha yao.
Mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini mheshimiwa Stephen Masele akiwa amebeba mtoto katika ofisi ya mtendaji wa kijiji cha Seseko inayotumika kama Zahanati ambapo kulikuwa kunatolewa huduma ya kliniki kwa watoto
Hapa ni katika shule ya Msingi Old Shinyanga iliyopo katika kata ya Old Shinyanga, Mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini mheshimiwa Stephen Masele akikagua choo kipya (kushoto) cha wanafunzi kinachojengwa chenye matundu 8 baada ya choo cha zamani kujaa na kuhatarisha maisha ya wanafunzi.
Mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini mheshimiwa Stephen Masele akiwa ndani ya choo kipya akiangalia ujenzi unavyoendelea.Kushoto kwake ni diwani wa tarafa ya Old Shinyanga mheshimiwa Picca Chogelo (CCM).
Mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini mheshimiwa Stephen Masele akizungumza nje ya choo hicho ambapo alisema mfuko wa jimbo umetoa shilingi milioni 2.3 kusaidia katika shughuli za maendeleo ya kata ya Old Shinyanga.
Mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini mheshimiwa Stephen Masele akiwa katika jengo la kituo cha Maendeleo ya awali ya watoto kilichojengwa na shirika la Save the Children kilichopo katika shule ya msingi Old Shinyanga katika kata ya Old Shinyanga
Diwani wa tarafa ya Old Shinyanga mheshimiwa Picca Chogelo (CCM) akielezea changamoto zilizopo katika kata ya Old Shinyanga wakati wa kikao cha mbunge Masele na wananchi wa eneo hilo ambapo alisema ni pamoja na uhaba wa matundu ya vyoo, katika shule,zahanati ya Old Shinyanga kukosa chumba kwa ajili ya akina mama wajawazito na eneo la zahanati kukosa uzio kutenganisha na mnada uliopo katika zahanati hiyo
Mbunge wa Shinyanga Mjini Mheshimwa Stephen Masele akizungumza wakati wa kikao na wananchi wa kata ya Old Shinyanga kujadili na kuzipatia ufumbuzi changamoto za wananchi.Masele alilipongeza shirika la Save the Children kujenga jengo kwa ajili ya maendeleo ya awali ya watoto katika kata hiyo na kwamba serikali itaendelea kusaidia katika miradi mbalimbali katika kata hiyo.Kushoto ni Katibu Mwenezi wa CCM Wilaya ya Shinyanga Mjini Rajabu Makuburi 
Mkazi wa Old Shinyanga akimwelezea Mbunge Masele jinsi wakazi wa eneo hilo wanavyoshinda na njaa kutokana na uhaba wa chakula inayochangiwa na chakula kuuzwa kwa bei kubwa
Mheshimiwa Masele akifurahia jambo na wanafunzi wa shule ya msingi Old Shinyanga
Mheshimiwa Masele akizungumza na baadhi ya vijana wa Old Shinyanga walioamua kuzuia gari lake asiendelee na safari ili asalimiane nao
Hapa ni katika shule ya Msingi Chibe katika kata ya Chibe manispaa ya Shinyanga.Aliyesimama ni ni Diwani wa tarafa ya Old Shinyanga mheshimiwa Picca Chogelo (CCM) akizungumza katika kikao cha mbunge na wananchi wa kata ya Chibe ambapo alisema kata hiyo haina shule ya sekondari watoto wanalazimika kusafiri umbali mrefu kwenda Old Shinyanga,eneo hilo halina huduma ya maji huku akiomba kata hiyo ijengewe barabara kwa kiwango cha lami kwani mji huo unakua kwa kasi
Mbunge wa jimbo la Shinyanga mjini Mheshimiwa Stephen Masele akizungumza na wakazi wa Chibe ambapo alisema anachofanya hivi sasa ni kuhakikisha shule zote za msingi katika jimbo lake zinamaliza changamoto ya uhaba wa matundu cha choo
Wananchi wa Chibe wakimsikiliza mbunge wao 
Wananchi wakiwa katika kikao
Hapa ni katika kata ya Lubaga: Katikati ni diwani wa kata ya Lubaga mheshimiwa Obeid Jilala (CHADEMA)akimpokea mheshimiwa Stephen Masele
Mheshimiwa Masele(CCM) akiwa na Obeid Jilala (CHADEMA) katika kikao cha kusikiliza na kutafuta ufumbuzi wa kero za wananchi
Diwani wa kata Lubaga mheshimiwa Jilala akimkaribisha mheshimiwa Masele (kushoto) ili azungumze na wananchi wa kata ya Lubaga.Kulia ni katibu mwenezi wa CCM wilaya ya Shinyanga mjini Rajabu Makuburi
Mheshimiwa Masele akizungumza katika kikao cha majadiliano kuhusu maendeleo ya kata ambapo alisema ametoa shilingi milioni moja kwa ajili ya kusaidia shughuli za maendeleo ya kata hiyo
Mheshimiwa Masele akijibu hoja ya ongezeko la bei kubwa ya maji na kero ya maji machafu yanayotoka kwenye mabomba ya maji ambayo yanasambazwa na SHUWASA
Kaimu Afisa Elimu wa manispaa ya Shinyanga Gideon Kyungai akielezea kuhusu namna serikali ilivyojipanga kukabiliana na changamoto ya uhaba wa walimu na matundu ya vyoo katika shule mbalimbali za manispaa ya Shinyanga
Hapa ni katika kata ya Chamaguha:Aliyesimama ni diwani wa kata hiyo Morice Mugini (CCM) akimkaribisha mheshimiwa Masele katika shule ya msingi Ushirika iliyopo katika manispaa ya Shinyanga
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Ushirika Lucia Amede akielezea changamoto ya matundu ya choo katika shule hiyo ambayo ina wanafunzi 844,matundu 6 pekee ya choo hali inayosababisha wanafunzi wapange foleni wakati wa kujisaidia
Mheshimiwa Masele alizungumza katika kikao na wakazi wa kata ya Chamaguha ambapo alisema amesema pia kuna pesa kutoka mfuko wa jimbo imetolewa kusaidia ujenzi wa choo kipya cha shule hiyo 
Katibu Mwenezi wa CCM wilaya ya Shinyanga Mjini Rajabu Makuburi akielezea jinsi ilani ya uchaguzi ya CCM inavyoendelea kutekelezwa katika kata mbalimbali za jimbo la Shinyanga
Mheshimiwa Masele akiangalia choo kipya inachojengwa katika shule ya msingi Ushirika
SIKU YA TATU KATIKA ZIARA YA MBUNGE STEPHEN MASELE-Hapa ni katika kata ya Kizumbi,pichani Kaimu Afisa Elimu wa manispaa ya Shinyanga Gideon Kyungai akizungumza katika shule ya msingi Kizumbi
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Kizumbi Neema Mkanga akitoa taarifa fupi kuhusu shule ya msingi Kizumbi kwa mbunge wa jimbo la Shinyanga mjini Stephen Masele.Alisema shule hiyo ina wanafunzi 502,matundu ya choo 6 ya wanafunzi,walimu 10 wanaotumia ambao hawana choo bali wanatumia tundu moja la choo cha wanafunzi
Katibu Mwenezi wa CCM wilaya ya Shinyanga Mjini Rajabu Makuburi akizungumza katika shule ya msingi Kizumbi 
Mheshimiwa Masele akizungumza na wananchi wa Kizumbi
Mheshimiwa Masele akisisitiza kuhusu huduma ya maji katika eneo hilo ambapo alisema huduma hiyo inatakiwa iwafikie kutokana na bomba la maji kupita eneo la kata hiyo
Mheshimiwa Masele akizungumza na wananchi wa Kizumbi
Mzee Paul Kashinje mkazi wa kijiji cha Bugayambele kata ya Kizumbi akiomba serikali iwapatie chakula kwani wanashinda na njaa kunywa uji 
Mheshimiwa akiwa katika eneo la choo cha shule ambacho kinatumiwa na walimu na wanafunzi,eneo hilo ndipo pia patajengwa choo kipya
Mheshimiwa Masele akiwasalimia wanafunzi wa shule ya msingi Kizumbi
Mheshimiwa Masele akiwa katika picha ya pamoja na walimu wa shule ya msingi Kizumbi
Hapa ni katika shule ya msingi Ibinzamata-Wanafunzi wakimpokea mheshimiwa Masele
Mheshimiwa Masele akiangalia matofali yanayotumika katika ujenzi wa choo cha shule ya msingi Ibinzamata
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Ibinzamata Vaileth Lumelezi akisoma risala kwa mheshimwa Masele ambapo alisema shule hiyo haina huduma ya umeme japo nguzo za umeme zinapita hapo.Alisema shule ina jumla ya wanafunzi 965 na matundu manne pekee ya choo
Mheshimiwa Masele akizungumza katika shule ya msingi Ibinzamata.Kulia kwake ni diwani wa kata ya Ibinzamata Reuben Kitinya
Wazazi wakimsikiliza mheshimiwa Masele
Mheshimiwa Masele akizungumza na wazazi wa wanafunzi
Hapa ni katika shule ya msingi Kitangiri katika manispaa ya Shinyanga,Pichani ni diwani wa kata ya Kitangiri Hamis Ngunila (CHADEMA) akimkaribisha mbunge wa jimbo la Shinyanga Mjini Stephen Masele ili azungumze na wakazi wa wanafunzi katika shule hiyo
Mwalimu mkuu wa shule ya msingi Kitangiri Chrizestom Kitale akisoma risala kwa mheshimiwa Masele ambapo alisema shule hiyo ina wanafunzi 1265,na kwamba inakabiliwa na uhaba wa madarasa na matundu ya vyoo
Mheshimiwa Masele akizungumza katika kikao hicho ambapo alisema ametoa shilingi milioni moja kusaidia maendeleo ya kata hiyo ikiwemo ujenzi wa matundu ya choo
Mheshimiwa Masele akizungumza na wazazi
Diwani wa Viti Maalum Mariam Nyangaka(CCM) akisisitiza jambo katika kikao hicho

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527