KIJANA AHUKUMIWA JELA MAISHA KWA KUNAJISI MTOTO WA MIAKA SITA



MAHAKAMA ya Wilaya ya Mlele, mkoani Katavi, imemhukumu kifungo cha maisha jela mkazi wa kijiji cha Kamsisi, tarafa ya Inyonga, Jilulu Lushinde (20) baada ya baada kupatikana na hatia ya kumnajisi mtoto wa miaka sita ambaye ni mwanafunzi wa darasa la kwanza katika Shule ya Msingi Imalauduki iliyopo wilayani humo.

Hakimu wa Mahakama ya Wilaya ya Mlele, Teotimus Swai ametoa hukumu hiyo leo baada ya kuridhishwa na ushahidi uliotolewa mahakamani hapo na upande zote mbili za mashitaka na utetezi.

Awali, Mwendesha Mashitaka Mkaguzi wa Polisi, Baraka Hongoli alisema mshitakiwa huyo alitenda kosa hilo Septemba 9, mwaka jana nyakati za jioni nyumbani kwa mtoto huyo anakoishi na wazazi wake.

Amesema siku ya tukio wakati wazazi wa mtoto huyo wakiwa wamekwenda harusini, mtoto huyo ambaye alibaki nyumbani kwao alivamiwa na kijana huyo na kumnajisi, hivyo kumsababishia maumivu makali katika sehemu zake za siri hali iliyosababisha kupiga kelele za kuomba msaada ndipo majirani walipojitokeza na kumuokoa.

Majirani hao walimkamata mtuhumiwa huyo na kutoa taarifa polisi, kisha kumpeleka mtoto huyo Kituo cha Afya Inyonga ambako ilithibitishwa amefanyiwa kitendo hicho hivyo kupatiwa matibabu.

Lushinde alishitakiwa kwa mujibu kifungu cha sheria 130 (1) (2) (e), lakini alikana shitaka hilo, huku upande wa Jamhuri ukiwa mashahidi wanne ambao walitoa ushahidi wao mahakamani hapo huku mtuhumiwa akijitetea mwenyewe.

Hakimu Swai amesema ushahidi uliotolewa mahakamani hapo pasipo na shaka umemtia hatiani kijana huyo, hivyo kwa kutumia kifungu cha 131 (1) sura ya 16 ya sheria iliyofanyia marekebisho 2002 mtuhumiwa anahukumiwa kwenda jela maisha.

Kwa mujibu wa sheria, mtoto chini ya miaka 10 adhabu zake ni kifungo cha maisha jela, hivyo ingawa mtuhumiwa aliiomba Mahakama impunguzie adhabu, ombi lake halikusikilizwa.
Via>>Habarileo

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527