ZITTO KABWE ADAI KUNA UPUNGUFU MKUBWA WA CHAKULA NCHINI..... SERIKALI YAPINGA


Wakati Mbunge wa Kigoma Mjini (ACT-Wazalendo), Zitto Kabwe akidai kuwa hali ya chakula nchini siyo nzuri kutokana na uhifadhi mbaya, Serikali imesema hali ni shwari licha ya baadhi ya maeneo kutopata mvua za wastani. 

Zitto alidai jana kuwa Ghala la Taifa la Chakula (SGR) lina hifadhi ya chakula kinachotosha kwa siku nane tu wakati Novemba 2015 kulikuwa na chakula cha kutosha miezi miwili. 

Kwa mujibu wa Zitto, taarifa ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) ya Novemba inaonyesha kuwa Mamlaka ya Taifa ya Hifadhi ya Chakula (NFRA), imebaki na tani 90,476 tu za chakula ambacho amedai ni cha kutosholeza siku nane.

 Hata hivyo, Waziri wa Kilimo, Mifugo na Uvuvi, Dk Charles Tizeba alijibu madai hayo ya Zitto akisema nchi ina chakula cha kutosha wala siyo cha siku nane wala mwezi pekee, bali zaidi. 


Dk Tizeba alisema NFRA inakuwa na akiba ndogo kwa kuwa mwaka 2016 ndiyo ambao nchi ilipata mavuno makubwa ya tani milioni 16 ambazo hazikuwahi kutokea, hivyo maghala ya watu bado yana akiba kubwa ya chakula hivyo wakala haukununua chakula kingi. 

“NFRA inanunua chakula kwa kuangalia mahitaji kwa mwaka huo ukoje, watu wakivuna sana maghala yao yanakuwa yamejaa na mahitaji ya chakula yanakuwa madogo ndiyo maana Serikali hainunui chakula kingi. Miaka miwili iliyopita Serikali ilinunua mahindi kwa wingi lakini yaliishia kuharibika,” alisema Dk Tizeba. 

Aliongeza kuwa Serikali sasa ina mradi wa kujenga ghala jingine lenye uwezo wa kuhifadhi tani 260,000 ili likiungana na la sasa lenye uwezo wa tani 246,000 nchi iwe na uwezo wa kuhifadhi tani zaidi ya 500,000. 

“Kuna maeneo mahindi yameanza kukomaa na wakulima wa huko watavuna kama kawaida, tunachokifanya tutadhibiti uuzaji wa chakula nje ya nchi bila vibali ili chakula kisambae zaidi kwa Watanzania. Japo siwezi kutaja kiasi cha chakula kilichopo kwa sababu za kiusalama, ila kinatosha siyo kwa siku nane wala mwezi mmoja bali ni zaidi,” alisema Tizeba. 

Juzi wakati akihutubia mkutano wa kampeni za udiwani katika kata ya Kiwanja cha Ndege, Manispaa ya Morogoro, Zitto alisema kauli ya Rais John Magufuli kwa wananachi wa Mkoa wa Kagera kwamba Serikali haina shamba ni kuficha uamuzi unaosababisha kukosekana kwa akiba ya chakula ya kutosha. 

Alidai kuwa hali ya chakula nchini si nzuri, wananchi wanashuhudia namna bei za vyakula zinavyopanda kila siku akidai kuwa bei ya sembe na mchele zimekuwa juu na gharama za maisha zitaendelea kupanda kutokana na uhaba wa chakula kuwa mkubwa.

 “Hali ya chakula inazidi kuwa mbaya kwa sababu ya maamuzi mabovu ya Serikali kuhusu hifadhi ya chakula. Serikali zote zilizopita huko nyuma zilikuwa zinanunua chakula cha akiba ili wakati wa ukame kama sasa chakula hicho kiingie sokoni, hivyo kushusha bei na kuwezesha wananchi kumudu gharama za chakula,” alisema Zitto. 

Aliongeza kuwa mpaka sasa NFRA ina tani 90,476 za chakula wakati kipindi kama hicho mwaka 2015 ghala la chakula lilikuwa na tani 459,561. 

Takwimu alizozitoa Zitto Kabwe alizinukuu katika ripoti ya BoT ya Novemba mwaka jana ambayo inaonyesha kuwa tangu Januari 2016 hadi Julai 2016, akiba ya chakula ilipungua kutoka tani 125,668 hadi 49,632, lakini hadi Oktoba mwaka huo iliongezeka hadi 90,476. 

Ripoti hiyo inaonyesha tofauti ya uhifadhi wa chakula kwa mwaka jana na miaka mingine miwili iliyotangulia kwani mwaka 2014 Januari, kulikuwa na tani 235,309 na Desemba, tani 466,583 huku mwaka mwaka 2015 Januari kukiwa na tani 459,561 na Desemba 180,746. 

Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Vikundi vya Wakulima Tanzania (Mviwata), Steven Ruvuga alisema hali halisi kwa wakulima siyo nzuri kwa kuwa mvua zilinyesha chini ya kiwango, hivyo kuna hofu ya ukosefu wa chakula cha kutosha baadaye. 

“Sasa hivi nipo Kiteto na kwa kawaida mahindi yalipaswa kuwa tayari yameinuka kufikia walau mabega ya mtu mzima, lakini nikiyatizama sasa bado yako chini. 

"Mwaka huu kuna hatari ya ukosefu wa chakula na naishukuru Serikali kwa kuwa imeanza kuchukua hatua katika maeneo yenye uhitaji,”alisema Ruvuga. 

Aliongeza kuwa Ghala la Taifa linapaswa kuwa na wastani wa tani 300,000 za akiba lakini kama sasa zipo 90,476 zinaweza zisikidhi mahitaji ya kila mtu hivyo ni vyema ikabuni mpango mbadala.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527