NDEGE YAUA WATU ZAIDI YA 30 BAADA YA KUANGUKIA NYUMBA

Watu zaidi ya 32 wamefariki baada ya ndege ya kubeba mizigo ya Uturuki, iliyokuwa safarini kutoka Hong Kong kuangukia nyumba za watu karibu na mji wa Bishkek nchini Kyrgyzstan.


Taarifa zinasema wengi wa waliokufa ni watu waliokuwa ardhini, ndege hiyo aina ya Boeing 747 ilianguka karibu na uwanja wa ndege wa Manas, takriban kilomita 25 kutoka mji mkuu Bishkek,


Nyumba zaidi ya 15 zimeharibiwa na watoto kadha wanaripotiwa kuwa miongoni mwa waliofariki. Imeelezwa kuwa hali ya hewa ilikuwa mbaya na kulikuwa na ukungu, ingawa chanzo hasa cha ajali hiyo hakijathibitishwa.


Kuna taarifa zinasema kuwa kwenye ndege hiyo kulikuwa na wahudumu wanne na mhudumu mmoja wa ndege amenusurika, watu kadhaa wamepelekwa hospitalini wakiwa na majeraha.


Msemaji wa huduma za dharura nchini humo Muhammed Svarov, ameambia AFP kwamba huenda idadi ya waliofariki ikaongezeka na juhudi za kuwasaka walionusurika zinaendelea.




Advertisement

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527