MUME AMUUA MKE WAKE KWA KUMPIGA NYUNDO KICHWANI AKIMTUHUMU KUCHEPUKA NA MWANAMME MWINGINE

Mwanamke mmoja mkazi wa Mikumi wilayani Keya, Mbeya aliyefahamika kwa jina la HILDA SIGARA  amefariki dunia akiwa anapelekwa Hospitali kwa matibabu baada ya kupigwa nyundo kichwani na mume wake aitwaye REBSON TWEVE umri kati ya miaka 30 – 35.

Kamanda wa polisi mkoani humo DCP Dhahiri Kidavashari amesema tukio hilo limetokea mnamo tarehe 05.01.2017 majira ya saa 12:00 asubuhi ambapo imedaiwa kuwa chanzo cha tukio hilo ni wivu wa kimapenzi kwani inasadikiwa mtuhumiwa alikuwa akimtuhumu marehemu kuwa ana mahusiano ya kimapenzi na mwanaume mwingine.

Amesema katika eneo la tukio kumekutwa nyundo moja, kisu kimoja na fimbo ya muanzi ambavyo vinasadikiwa kutumika katika tukio hilo.

Mwili wa marehemu umehifadhiwa Hospitali ya Wilaya Kyela ukisubiri kufanyiwa uchunguzi wa kitabibu na upelelezi unaendelea huku mtuhumiwa akiwa ametoroka mara baada ya tukio na juhudi za kumtafuta zinaendelea.

Aidha, katika matukio mengine kamanda huyo amesema kuwa jeshi la polisi limepokea taarifa za kujinyonga kwa watu wawili ambao miili yao imekutwa ndani ya nyumba zao katika maeneo tofauti.

Watu hao ni pamoja EDWARD PETER  mfanyabiashara na Mkazi wa Majengo na aliyekutwa amekufa chumbani kwake huku mwili wake ukiwa hauna majeraha yoyote, na mwingine ni ROBERT MWAISENYE Mkazi wa Mbugani wilayani Chunya ambaye alikuwa amejinyonga kwa kutumia kamba ya manila akiwa ndani ya nyumba yake.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527