MTUNZA BUSTANI AFIKISHWA MAHAKAMANI KWA KUMTUKANA RAIS MAGUFULI NA MAKAMU WA RAIS

Mtunza bustani Maganga Masele, amefikishwa kwenye Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, Jijini Dar es salaam kwa tuhuma za kutoa lugha ya matusi dhidi ya Rais John Magufuli na Makamu wa Rais Samia Suluhu Hassan kuhusu utendaji wao wakuliongoza taifa.


Wakili wa Serikali Lucy Mallya amesema kuwa Desemba 22, mwaka jana Masele akiwa Leaders Club Kinondoni jijini Dar es salaam, alitoa lugha ya matusi dhidi ya Rais Magufuli na Samia, maneno ambayo yangeweza kuleta uvunjifu wa amani.


Hata hivyo baada ya kusomewa mashtaka hayo, Masele alikana kuhusika na tuhuma hizo, ambapo Mallya alidai kuwa upelelezi haujakamilika pia hakuna pingamizi la dhamana kwa kuwa kisheria kosa hilo linadhaminika.


Kwa upande wake Hakimu Mwijage amesema kuwa ili mshitakiwa awe nje kwa dhamana ni lazima awe na mdhamini mwenye barua yenye utambulisho atakayesaini bondi ya sh 500,000.


Masele amekamilisha masharti na kuachiwa kwa dhamana,na kesi yake itatajwa Januari 24

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527