SERIKALI YAANZA KUHAKIKI VYETI VYA NDOA KWA WATUMISHI WA UMMA

Gazeti la Tanzania Daima limeripoti kuwa Serikali imeanza uhakiki wa vyeti vya ndoa kwa watumishi wa umma.

 
 Hatua hiyo ambayo imewashtua watumishi wengi wa umma, imeelezwa kuwa ni mwendelezo wa harakati za Serikali ya Rais John Magufuli kuhakiki watumishi wa umma ili kuondokana na watumishi hewa.



Wakati Serikali ikianza na uhakiki wa vyeti vya ndoa, kazi ya uhakiki wa watumishi hewa na vyeti vyao vya elimu inaendelea sehemu mbalimbali nchini. 



Kwa muhibu wa Gazeti hilo, habari ambazo limezipata zinasema kuwa serikali imeanzisha uhakiki huo nchi nzima kwa madai kuwa baadhi ya watumishi wa umma wamekuwa wakitoa taarifa za uongo kwamba wana ndoa ili kupata nauli na stahiki zingine za likizo wakati hawana ndoa. 



Habari zaidi zinasema kuwa walimu wakuu wa shule zote za Wilaya ya Ilala wamepewa siku mbili kutekeleza agizo hilo kwa walimu wao. 



Mmoja wa walimu hao ambaye ameomba jina lake lihifadhiwe, alilithibitishia Tanzania daima kuwa ametoa siku mbili kwa walimu wa shule yake wenye vyeti vya ndoa waviwasilishe kwake.



"Kweli tumepewa agizo hilo leo manispaa ya Ilala na tumetakiwa kuwasilisha vyeti hivyo kesho na tayari baadhi ya walimu wangu wamefanya hivyo leo na kesho zoezi hilo linakamilika"



Alipoulizwa sababu ya kuwepo kwa zoezi hilo, mwalimu huyo alisema hajui lakini anahisi lina lengo la kudhibiti taarifa za uongo za watumishi wakati wa kuomba likizo. 



Wakati walimu wa shule za Ilala wakitakiwa kuwasilisha vyeti vyao vya ndoa, wilaya nyingine za Temeke, Kinondoni, Ubungo na Kigamboni hawana taarifa hizo. 



Mmoja wa walimu kutoka Manispaa ya Ilala alisema kuwa uhakiki huo una lengo la kutaka kuchelewesha zaidi malipo na stahiki za walimu za likizo ambazo hazijalipwa kwa miaka mingi.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527