BONDIA THOMAS MASHALI KUAGAWA LEO LEADERS,KUZIKWA KINONDONI

 
MWILI wa bondia wa ndondi za kulipwa nchini, Thomas Mashali aliyeuawa Kimara jijini Dar es Salaam usiku wa kuamkia Jumatatu, utazikwa leo kwenye makaburi ya Kinondoni.

Baba mzazi wa marehemu, Malifedha Mashali alisema kuwa mwili wa mtoto wake huyo aliyeuawa kwa kupigwa na watu wasiojulikana, utazikwa katika makaburi ya Kinondoni Mwembejini.

Alisema mipango mingine ya mahali utakapoagiwa mwili huo na utakapoombewa, bado ilikuwa inaendelea na alikuwa hajajua shughuli hizo zitafanyikia wapi.

Mzee Mashali alisema kuwa mwili wa mtoto wake utaagwa katika viwanja vya Leaders Club Kinondoni kuanzia saa 4:30 asubuhi kabla ya kwenda kulazwa katika nyumba yake ya mileleni katika makaburi ya Kinondoni mapema mchana.

Mashali alikuwa akishikilia mikanda ya WBO na UBO kabla ya kifo chake, ambapo amekufa huku akiacha mataji kibao ya ngumi ya hapa nchini na yale ya kimataifa.

Wadau wengi wa michezo walitoa masikitiko yao kuhusu kifo hicho cha Mashali huku wengi wao wakisema kuwa bondia huyo alikuwa na kipaji cha aina yake katika ndondi.

Mashali alizaliwa Dar es Salaam mwaka 1989 na alianza kupigana ngumi za kulipwa Novemba 27, 2009 alipopigana na kumtwanga Hamadu Mwalimu katika pambano lililofanyika katika ukumbi wa Texas, Manzese

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527