Utajiri wa Sh. Bilioni 8 wa Mwanamuziki Diamond Wazua Maswali

Hivi karibuni, Mtandao wa The Net Worth (www.the-net-worth.com) umetangaza utajiri wa staa wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ (26) ambapo kwa mujibu wa jarida hilo, nyota huyo ana utajiri wa dola milioni 4 za Kimarekani (sawa na zaidi ya shilingi bilioni 8.75), jambo lililozua maswali yapatayo 6 miongoni mwa Wabongo.

Mtandao huo umekuwa ukijipambanua kwa kuanika utajiri wa watu maarufu barani Afrika wakiwemo David Adedeji Adeleke ‘Davido’ (shilingi bilioni 32), Ayodeji Balogun ‘Wizkid’ (bilioni 24) na wengineo kibao.

Baadhi ya wasomaji wa gazeti hili wameuliza maswali hayo wakisema mwenye uwezo wa kuyajibu ni Diamond mwenyewe na si jarida hilo huku wakitia shaka kwamba, huenda waandaaji wa jarida hilio wamepewa taarifa za uongo na Diamond mwenyewe.

AMEPATA WAPI UTAJIRI HUO WA HARAKA?
Swali la kwanza ambalo wengi waliosikia taarifa za mtandao huo walihoji, nini chanzo cha utajiri huo kwani wengi wanaamini kwamba hata kama soko la muziki wa kizazi kipya linalipa, haliwezi kuwa katika kiwango cha kumfikisha Diamond au Dangote katika utajiri huo.

“Kwanza nyie waandishi mjue mtandao unaposema Diamond ana utajiri wa kufikia shilingi bilioni nane ina maana anaingiza bilioni moja na ushee kila mwaka, maana Diamond kushika soko la muziki hasahasa kwa maana ya kuitwa kufanya shoo za pesa nyingi ni kuanzia mwaka 2010.

“Haiwezekani! Hata kama ni huo muziki ndiyo pesa zote hizo? Kwani anafanya shoo ngapi kwa mwaka mzima? Lazima kuna namna hapa. Anaweza kuwa jipu huyu, tunamuomba Magufuli amchunguze,” alisema msomaji mmoja aliyeomba hifadhi ya jina lake.

MTANDAO WAMCHANGANUA
Kwa mujibu wa mtandao huo, Diamond anatajwa kwamba analipwa wastani wa shilingi milioni saba na nusu kwa kila shoo. Japokuwa mwenyewe amekuwa mgumu wa kueleza kiwango anacholipwa kwa kila shoo, lakini uchunguzi wa gazeti hili umebaini kuwa, huwa inategemea aina ya shoo anayotumbuiza.

KAMA NDIYO HIVYO
Msomaji huyo akaendelea: “Kama utafiti wa mtandao huo ni wa kweli, Diamond kila wikiendi anaingiza shilingi 7, 500,000 si ndiyo? Na mwezi mmoja una wikiendi nne, hivyo anaingiza shilingi 30,000,000 kwa mwezi mmoja yaani 7,500,000 mara wiki nne.

“Sasa mwaka una wikiendi ngapi? Chukua mwezi mmoja milioni 30, mara miezi 12 ni sawa na shilingi milioni 360. Na yeye yuko kwenye gemu tangu 2010. Kwa hiyo kwa miaka hii sita tu ametengeneza vipi pesa za kufikia bilioni moja na zaidi kila mwaka mpaka kuwa na bilioni 8 na kadhaa?


“Unaweza kusema kuna pesa za mikataba ya kampuni za simu, lakini pia mjue hapo kuna kununua magari yake yale, kujenga nyumba Madale. Kujiachia na akina Wema (Sepetu), kumuuguza mama yake na kufanya mambo kadha wa kadha! Hapo tunadanganyana jamani.”

ANALIPA KODI KIHALALI?
Baadhi ya wasomaji pia waliuliza swali jingine ambalo wengi wameendelea kutaka kujua je, kama utajiri wake anaupata kwa njia halali, analipa kodi ya mapato (TRA) kama sheria inavyotaka? Ni kawaida kwa wasanii wakubwa hasa kwa nchi zilizoendelea, kulipa kodi katika kila shughuli za kuingiza kipato wanazozifanya.

Kwa mfano, katika kila shoo anayopiga, Diamond anapaswa kulipia kiwango cha kodi kulingana na kiasi cha fedha alichoingiza.

“Kama kweli hakuna figisufigisu kwenye utajiri wake, atuambie huwa analipa kodi? Mara ya mwisho alilipa lini na alilipa kiwango gani? Huyu jamaa anatakiwa kumulikwa, huenda kuna dili nyingine zinazomuingizia fedha kwa njia zisizo halali halafu anasingizia muziki,” alichangia mchangiaji mmoja kwenye mtandao wa kijamii wa Facebook.

ANAUZA MADAWA YA KULEVYA?
Wapo waliokwenda mbele zaidi na kumhusisha Diamond na biashara haramu ya madawa ya kulevya ‘unga’ kwamba huenda anajishughulisha na biashara hiyo ndiyo maana ‘ametusua’ haraka wakitolea mfano wa Juni mwaka jana alipotaitiwa Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA), jijini Dar ambapo walinzi wa uwanja huo walimtilia shaka na kumpekua kutokana na safari zake za mara kwa mara nje ya nchi lakini hakukutwa na unga.

“Unajua hawa wasanii siku hizi wanashiriki sana kwenye biashara ya unga. Wengi wakiwa wanasafirisha madawa wanasingizia kwamba wanakwenda kufanya shoo, mara Afrika Kusini, mara Dubai, Marekani na nchi za Ulaya.

“Diamond siku hizi amekuwa na ‘ruti’ nyingi sana za nje ya nchi, huenda anauza ‘ngada’. Haiwezekani mtoto mdogo awe na fedha nyingi kiasi hicho,” Michael Sabuni, mkazi wa Ubungo- Maziwa, Dar aliliambia gazeti hili kwa njia ya simu.

ANAHUSIKA NA FREEMASON?
Yapo madai mengine kwamba msanii huyo ni mwanachama wa jamii ya siri ya Freemason inayotajwa kuwapatia utajiri wafuasi wake kwa njia ya makafara na nguvu za giza madai ambayo baadhi ya wasomaji wameyaibua tena kufuatia mtandao huo kumtaja Diamond kwamba anamiliki bilioni 8 kibindoni.

“Mbona kitambo tu watu wanamhisi jamaa kwamba ni Freemason? Unajua ukishajiunga na hawa watu halafu ukafuata masharti yao ya kutoa kafara, kuua watu na kumuabudu shetani, utajiri upo nje nje. Inawezekana hao ndiyo wanaompa jeuri kwa sababu mimi siamini kama fedha zote hizo amezipata kwa sababu ya muziki tu,” alichangia msomaji wetu aliyepiga simu chumba cha habari baada ya kuona taarifa hizo za utajiri wa Diamond mtandaoni.

ANAMTUMIA MWANAYE KAMA KITEGA UCHUMI?
Yapo madai mengine kwamba utajiri wa Diamond unachangiwa kwa kiasi kikubwa na mwanaye aliyezaa na mwanamama Zarina Hassan ‘Zari The Boss Lady’, Latiffa ‘Tiffa’, kwamba tangu kuzaliwa kwa mtoto huyo, makampuni mengi, hasa yanayohusika na biashara ya bidhaa za watoto na mitandao ya simu, yamekuwa yakimlipa mamilioni ya fedha kwa sababu ya kumtumia mtoto huyo kwenye matangazo ya bidhaa zao.



ANAHONGWA NA ZARI?
Swali jingine ambalo wengi wanajiuliza ni kama msanii huyo anahongwa fedha na mpenzi wake, Zari ambaye kabla ya kuanzisha naye uhusiano wa kimapenzi, alikuwa mke wa tajiri wa Kiganda, Ivan Ssemwanga mwenye makazi yake nchini Afrika Kusini.

“Hakuna cha muziki wala nini, unajua Ivan amemuachia utajiri mkubwa sana mkewe kule Sauzi (Afrika Kusini), anamiliki vyuo mbalimbali, maduka ya urembo na magari mengi ya kifahari. Yeye ndiye anayempa jeuri Diamond, mbona ipo wazi kabisa?” alisema mchangiaji mwingine aliyeomba hifadhi ya jina lake.

MAMA YAKE ANAJUA KILA KITU
Baadhi ya wasomaji walisema kuwa, mama wa Diamond ndiye anayejua utajiri wa mwanaye unatokana na nini kwani inadaiwa kuwa ndiye mwongozaji wake mkubwa.

“Mimi naamini mama Diamond anajua mengi sana. Hawa wamama wa mastaa wamekuwa ndiyo nguzo ya watoto wao kupata pesa. Tunaweza kuumiza vichwa anapata wapi utajiri kumbe mama yake anajua,” alisema msomaji, Isaya Mwarami wa Mabibo, Dar.

DIAMOND ANASEMAJE?
Baada ya kusikia madai hayo ya watu mbalimbali waliokuwa wakiuzungumzia utajiri wa Diamond, gazeti hili lilimtafuta Dangote mwenyewe na kumsomea maswali yote sita ambapo aliguna na kuanza kuyajibu kwa kifupi:

“Sikia braza, hayo wanayoyasema Wabongo hayana ukweli wowote lakini kwa sababu ni kawaida ya Waswahili kuongea mimi nafikiri waache waendelee kuongea lakini ukweli ni kwamba muziki wangu ndiyo ulionifikisha hapa nilipo.

“Nafanya kazi kwa bidii, narekodi ngoma kali, nafanya video zilizokwenda shule, namtanguliza Mungu kwa kila jambo, nina nidhamu ya fedha na sihusiki kwa namna yoyote ile na kujiingizia kipato kwa njia zisizo halali.

“Mimi nafuata sana sheria, ishu ya kulipa kodi, unajua promota anayeandaa shoo ndiye anayetakiwa kusimamia kila kitu. Kwa hiyo mimi akinipa changu, anakuwa tayari ameshakata kodi na mambo ya vibali na kila kitu.

“Ishu ya Freemason siyo kweli bwana, unajua baadhi ya Wabongo wanapenda sana kunizushia mambo. Kuna kipindi walikuwa wanasema natumia uchawi, wameona haitoshi wananizushia Ufreemason na mengine mengi, hakuna kitu kama hicho.

“Nina hofu ya Mungu na yeye ndiye anayeniongoza katika kila ninachokifanya. Mama yangu anajua napata fedha kwa sababu ya kujituma kwangu na si vinginevyo.”

UTAJIRI WAKE MWAKA 2013
Mwaka 2013, alipohojiwa na mtangazaji Zamaradi Mketema wa Clouds TV kwenye Kipindi cha Take One, Diamond alisema utajiri wake, ikiwa ni pamoja na vitega uchumi vyote na fedha zilizopo benki ni zaidi ya shilingi bilioni moja (ikaandikwa kwenye Magazeti Pendwa ya Global Publishers), lakini miaka mitatu baadaye (2016), kwa mujibu wa mtandao huo, utajiri wake umepaa hadi kufikia shilingi bilioni 8.

MALI ZAKE ZA MACHONI
Mpaka sasa, Diamond anamiliki nyumba kubwa ya kifahari iliyopo Madale ambayo inakadiriwa kuwa na gharama ya shilingi bilioni moja. Pia ametumia kiasi kinachoaminiwa kufikia shilingi milioni mia moja kukarabati nyumba ya familia iliyopo Tandale, Dar. Inaelezwa pia kuwa anazo nyumba nyingine mbili zilizopo Kijitonyama na nyingine iliyopo Mwananyamala.

Ana magari matatu, BMW, Toyota Land Cruiser Prado na Toyota Harrier. Anamiliki daladala kadhaa zinazofanya safari zake ndani ya Jiji la Dar na Bajaj. Pia ana mikataba na Kampuni za Vodacom, Samsung, Cocacola na nyinginezo.

Chanzo:Global Publishers

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527