Ni Balaa!! DIAMOND,MASANJA,JOTI NA WASANII WENGINE KIBAO KUCHUNGUZWA NA POLISI ISHU YA MADAWA YA KULEVYA

KIMENUKA! Jeshi la Polisi Tanzania kwa kushirikiana na taasisi mbalimbali za serikali zimeanza kuwachunguza watu wenye majina makubwa ‘mastaa’ Bongo ambao wameibuka na utajiri wa ghafla, Uwazi limeambiwa.

Masanja Mkandamizaji.
Kwa mujibu wa chanzo nyeti ambacho kiko ‘jikoni’ kwenye jeshi hilo, mbali na mastaa, wengine ambao tayari orodha yao ipo ni wafanyabiashara, wafanyakazi wa serikali na viongozi wa dini ambao wameibuka kuwa mamilionea kwa muda mfupi huku shughuli zao za wazi zikiwa haziwezi kuwatajirisha.

Madawa ya kulevya.
BIASHARA YA MADAWA YA KULEVYA NDIYO KIINI CHA YOTE

Chanzo: “Imeonekana kuwa mastaa wengi wanaibuka kuwa na utajiri siku hizi, huenda wanajihusisha na kusafirisha madawa ya kulevya.

“Ndiyo maana wengi wao kila kukicha, mara wapo China, mara India, wengine wanakwenda mpaka Thailand. Hao wanachunguzwa kwa mtindo wa nyendo, kila mmoja ambaye yumo kwenye orodha ya jeshi amewekewa askari wawili wa kumfuatilia.”

KUKAMATWA

Chanzo hicho kikaendelea kusema kuwa wale ambao watathibitika kwamba biashara zao za wazi haziwezi kutoa utajiri wa ghafla watakamatwa na kuhojiwa.

DIDA AMESHAKAMATWA, AMESHAHOJIWA

Chanzo hicho kilieleza kuwa katika oparesheni hiyo maalum, watu kumi wameshakamatwa, akiwemo Mtangazaji wa Kituo cha Redio cha Times FM, Hadija Shaibu ‘Dida’.

“Watu kumi tayari wamekamatwa na kuhojiwa. Yumo yule mtangazaji Dida wa Mchops (siku hizi si wa Mchops). Saba wamekwenda na maji, watatu akiwemo Dida waliachiwa baada ya kuthibitika kwamba mali zao ni halali,” kilisema chanzo.

IKOJE KWA VIONGOZI WA DINI?

Chanzo kilisema kuwa kuhusu viongozi wa dini ambao nao wameibuka kuwa matajiri wa kutupwa, wamejenga mahekalu ya maana, nao wanachunguzwa na kati ya watu kumi waliokamatwa, yumo mchungaji mmoja (hakumtaja jina) ambaye aliachiwa.

“Lakini orodha ya hawa ni ndefu, kumbe wengi wanajihusisha na kuuza madawa ya kulevya. Nao wamewekewa askari wawiliwawili ambao wanaingia hadi kwenye ibada zao lakini wenyewe hawajui,” kilisema chanzo. 

JOTI WA KOMEDI  ATAJWA

Katika hali ya kushangaza, chanzo hicho kilidai kuwa staa ambaye alikuwemo kwenye orodha na akafuatiliwa na kuachiwa ni msanii wa Kundi la Orijino Komedi, Lucas Mhuvile ‘Joti’ ambapo ilidaiwa hakuonekana kuwemo kwenye cheni ya wauza unga nchini.

“Lakini hata hiyo orodha nyingine si kwamba wamehukumiwa kuhusika kufanya biashara hiyo ila wanachunguzwa,” kilisema chanzo hicho.

YAMEKUJAJE?

Hatua hiyo, kwa mujibu wa chanzo, imekuja kufuatia madai ya wananchi wengi kwamba matajiri waliopo mtaani wengi ni wauza unga ambao hufanya biashara hiyo waziwazi, wengine wakisema kuna polisi wanaojua kila kitu lakini kwa sababu wanakatiwa kitu kidogo wanawalinda.

“Si kwamba serikali haitaki watu wawe  na maendeleo makubwa, bali utajiri wao uwe wa wazi wenye vielelezo vinavyokubalika. Kwa sasa vijana wengi wakiwemo wasanii na wachezaji wanashindana kwa utajiri lakini baadhi yao ndiyo hivyo tena wamegundulika wanajihusisha na biashara ya madawa ya kulevya, wengine wamekamatwa nje ya nchi na wanakabiliwa na hukumu ya kifo,” kiliongeza chanzo hicho.

UWAZI LAWASAKA WALIOIBUKA NA UTAJIRI

Kama kigezo kikubwa ni utajiri wa ghafla, Uwazi liliwasaka mastaa ambao walishaandikwa na Magazeti Pendwa ya Global Publishers (likiwemo Uwazi lenyewe).

DIDA

Katika Gazeti la Ijumaa Wikienda toleo la wiki mbili nyuma kulikuwa na kichwa cha habari ukurasa wa mbele; UTAJIRI WA DIDA GUMZO.

Katika habari hiyo Dida alisema:

“Mimi sipendi kuanika vitu ninavyomiliki ila ni kweli nina nyumba mbili, moja Kigamboni na nyingine Goba ya gorofa. Magari ninayo matatu, hilo Vogue mchakato unaendelea, ukikamilika nitaliingiza nchini.

 “Kuhusu miradi yangu mingine siwezi kuianika hadharani kwa sababu, kwanza sipendi kabisa mambo hayo.”

Hata hivyo, Dida alikiri kukamatwa Machi, mwaka huu na kuhojiwa kisha kuachiwa. Alikuwa anakwenda Hong Kong, China.

MASANJA

Katika Gazeti la Risasi Mchanganyiko la Jumatano ya Aprili 2, 2014 ukurasa wa mbele kulikuwa na kichwa cha habari; UTAJIRI WA MASANJA KUFURU.

Masanja alipoulizwa alikoupata utajiri huo alisema: “Ni kweli nina nyumba tatu hapa mjini, kampuni ya ulinzi na mashamba ya mpunga ekari 50 nyumbani Mbarali, Mbeya. Kuhusu magari pia ni kweli kabisa. Mimi ni mtumishi sitakiwi kusema uongo. Orijino Komedi ndiyo chanzo cha vyote, pale ndipo kwenye koki.”

DIAMOND

Katika Gazeti la Ijumaa Wikienda toleo la Julai 29, 2013 ukurasa wa mbele kuliandikwa; DIAMOND ANUNUA MTAA.

Diamond (Nasibu Abdul) alipoulizwa alikiri na kusema: “Muziki ndiyo chanzo kikubwa. Najua (nyumba) zitanisaidia endapo muziki wangu utakosa soko. Mimi na mama yangu (Sanura Kassim ‘Sandra’) tuliishi kwa dhiki sana na sasa kwa kipindi hiki ambacho Mungu ananisaidia na kuniwezesha kupata fedha kwa wingi, siwezi kuishi maisha ya anasa ya kununua magari ya kifahari bali najenga nyumba.”

KAJALA MASANJA

Kwa upande wake, Kajala ambaye aliwahi kuandikwa na Gazeti la Amani likiwa na kichwa; KAJALA AIBUKA TAJIRI GHAFLA, alipoulizwa alisema:

“Sina utajiri wa ghafla bali namtegemea Mungu, natengeneza filamu naweka pesa ndiyo maana naweza kufanya makubwa.”

DK. CHENI

Staa wa filamu Bongo, Muhsin Awadh ‘Dk. Cheni’ hakupatikana katika simu na marafiki zake walisema yupo safarini nchini China.

VICKY KAMATA

Huyu ni Mbunge wa Viti Maalum (UVCCM), Geita. Aliandikwa na Gazeti la Uwazi la  Februari 18, mwaka huu kwa kichwa; UTAJIRI WA VICKY KAMATA BALAA.

Katika mahojiano na Uwazi kuhusu utajiri wake, Vicky alisema: “Mafanikio yote yametokana na juhudi zangu za kujituma katika kufanya kazi, namwamini Mungu siku zote. Hakuna dhambi mbaya hapa duniani kama kukata tamaa. Tukifanya kazi kwa kujituma na kumwamini Mungu hakuna Mtanzania maskini.”

GWAJIMA

Mchungaji Josephat Gwajima wa Kanisa la Ufufuo na Uzima yeye aliandikwa kwa kuchanganywa na utajiri wa wenzake wengine. Lakini alipohojiwa alisema:

“Mali nilizonazo ni kutokana na jitihada zangu kwani mimi ni mwalimu, nimekuwa nikisafiri kwenda nchi za Ulaya kufundisha na huwa nalipwa fedha nyingi, pia mali zingine ikiwemo gari la Hummer nilipewa na marafiki zangu, mali zingine ni za kanisa.”

MZEE WA UPAKO

Katika Gazeti la Uwazi la Desemba 11, 2012, Lusekelo Anthony ‘Mzee wa Upako’ wa Kanisa la Maombezi, aliandikwa kwa kichwa; UTAJIRI WA MZEE WA UPAKO NI KUFURU.

Alipohojiwa, alisema: Magari yote nimeandika kwa jina langu ili niyalipie kodi, situmii mwamvuli wa kanisa kwa kukwepa kodi.

“Kila mtu anatakiwa kuwa tajiri lakini utajiri wa halali siyo ule wa kudhulumu, ndiyo maana naweza kusimama hapa madhabahuni na kutaja mali zangu, magari hayo si mali ya kanisa ni yangu.”

KAMANDA NZOWA

Uwazi lilimsaka Kamanda wa Kikosi cha Kupambana na Kuzuia Madawa ya Kulevya Tanzania, Godfrey Nzowa ambapo alikiri kuwachunguza watu wengi ambao majina yao yamepelekwa na wananchi au wametajwa na watuhumiwa wengine ambao wameshakamatwa.

“Hapa tuna majina ya watu wengi wa aina mbalimbali wakiwemo viongozi wa dini, wasanii, viongozi wa serikali na wafanyakazi wa taasisi za serikali na zisizo za serikali. Hawa ni wale ambao wameibuka kuwa matajiri ghafla.

“Siwezi kukutajia majina yao kwa sababu mambo haya yanafanyika kwa siri kwani hawa watu ni wajanja sana, kwa sasa vita hii si yangu tu bali ni ya task force, wananchi na dunia kwa jumla, kwa kweli kuna orodha ndefu na hili zoezi si la muda mfupi ni endelevu,” alisema Kamanda Nzowa.

GPL

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments