Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

NAIBU KATIBU MKUU MITAWI AIPONGEZA ATCL KWA MAFANIKIO, AITAKA KUONGEZA UBUNIFU NA USHINDANI




Naibu Katibu Mkuu wa Wizara ya Uchukuzi, Bw. Abdallah Mitawi, ameipongeza Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL) kwa mabadiliko makubwa na hatua za maendeleo iliyopiga kwa kipindi kifupi tangu kuanzishwa kwake, ikiwemo kuongeza idadi ya ndege hadi kufikia 16 na kupanua mtandao wa safari hadi kufikia vituo 17 ndani ya Tanzania na 20 nje ya nchi

Amesema hayo jijini Dar es Salaam wakati wa ziara yake katika Kampuni hiyo, ambapo alipokea taarifa kuhusu utekelezaji wa majukumu, mafanikio na mipango ya maendeleo ya ATCL

Bw. Mitawi amesema ongezeko la mapato ya Kampuni hadi kufikia takribani Shilingi bilioni 700 katika mwaka wa fedha 2025/26 ni mafanikio makubwa yanayopaswa kuendelezwa kwa kuongeza ufanisi, tija na ubora wa huduma

Ameitaka ATCL kuendelea kuwa bunifu, kutumia ipasavyo teknolojia katika shughuli zake na kuimarisha ushirikiano na mashirika ya ndege ya kikanda na kimataifa ili kuongeza ushindani, kupanua masoko na kuimarisha nafasi ya Tanzania katika soko la usafiri wa anga


Aidha, Naibu Katibu Mkuu ameitaka ATCL kuchukua tahadhari na kujiandaa mapema kukabiliana na changamoto zinazoweza kujitokeza kutokana na mvua kubwa zinazotarajiwa za El Nino na kuongeza kuwa kutokana na umuhimu wa usafiri wa anga katika shughuli za kiuchumi na kijamii, ni muhimu Kampuni kuimarisha mifumo ya utayari na kuchukua hatua za mapema kuhakikisha athari zinazoweza kujitokeza zinapunguzwa, huku usalama na mwendelezo wa huduma ukiendelea kupewa kipaumbele

Kwa upande wake, Mkurugenzi Mtendaji wa ATCL, Mha. Peter Ulanga, amesema Kampuni imeendelea kutekeleza mikakati ya kupanua mtandao wa safari, kuongeza mapato na kuimarisha ushirikiano wa kibiashara na mashirika ya ndege ya kimataifa ambapo hadi sasa ATCL imefikia ushirikiano na mashirika 15 ya nje ya nchi, hatua inayolenga kuongeza fursa za biashara, kuboresha muunganiko wa safari na kuimarisha nafasi ya Tanzania katika mtandao wa usafiri wa anga kikanda na kimataifa.










Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundeblog@gmail.com