Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

SHIRIKA LA GIFTED NATURE (GIFTED NATURE NGO) NA MRADI WA ‘SHUJAA PATH’

Na Mwandishi Wetu

SHIRIKA lisilo la kiserikali la Gifted Nature NGO limeanzisha programu maalumu ya ‘Shujaa Path’ inayolenga kuwawezesha wavulana na vijana wa kiume kukabiliana na changamoto mbalimbali za kijamii, kielimu na kiuchumi ili kujenga maisha yenye tija na endelevu.

Gifted Nature NGO, lililoanzishwa Tanzania mwaka 2021 na Dk Sophia Mfaume Kizigo, linajikita katika kuwawezesha wananchi, kulinda mazingira na kutengeneza fursa kwa vijana ili waweze kutumia uwezo na vipaji vyao katika kujenga maisha bora.

Kupitia programu zake mbalimbali zinazolenga jamii, shirika hilo hushughulikia changamoto za kijamii na kimazingira huku likihamasisha elimu, uongozi, ukuzaji wa ujuzi, uwajibikaji na ushiriki wa wananchi katika shughuli za maendeleo.

Miongoni mwa programu hizo ni Shujaa Path, iliyoanzishwa mwaka 2025 kwa lengo la kuwafikia wavulana na vijana wa kiume ambao mara nyingi hawapati uangalizi wa kutosha katika programu mbalimbali za maendeleo.

Kwa mujibu wa Gifted Nature, programu hiyo imeanzishwa baada ya kubaini changamoto zinazowakabili vijana hao, zikiwemo kuacha shule au kutoshiriki kikamilifu katika elimu, ukosefu wa malezi na ushauri wa kitaalamu, ukosefu wa ajira na fursa za kiuchumi pamoja na ushawishi hasi kutoka kwa rika.

Changamoto nyingine ni ukosefu wa mazingira rafiki kwa vijana hao kukuza vipaji, uwezo na vipawa walivyonavyo.

Kupitia kaulimbiu yake “Every Boy, A Shujaa – Kila Kijana wa Kiume ni Shujaa,” Shujaa Path inalenga zaidi ya kutatua changamoto zinazowakabili wavulana, bali kuwasaidia kutambua thamani na uwezo wao katika jamii.

Programu hiyo pia inalenga kuwajengea vijana kujiamini, maadili mema na ujuzi muhimu wa maisha, huku ikiwaandaa katika maeneo ya ujasiriamali, ajira na uongozi ili waweze kuwa raia wenye mchango chanya katika familia na jamii zao.

Gifted Nature inaamini kuwa kumjenga kijana leo ni kujenga jamii bora ya kesho, hivyo imeweka mkazo katika ushirikiano na Serikali, shule, jamii, wadau wa maendeleo, sekta binafsi pamoja na vyombo vya habari.

Kupitia ushirikiano huo, shirika hilo linalenga kuendeleza na kupanua Shujaa Path ili kuwafikia wavulana na vijana wengi zaidi katika maeneo mbalimbali nchini Tanzania.

Lengo kuu ni kuhakikisha vijana wa kiume wanapata fursa sawa za kujifunza, kukuza vipaji, kupata ujuzi na kushiriki kikamilifu katika shughuli za maendeleo ya familia, jamii na Taifa.







Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundeblog@gmail.com