MZEE WA UPAKO : TAJENI NILIKUNYWA POMBE AINA GANI,BAR GANI

Mchungaji wa Kanisa la Maombezi (GRC), Anthony Lusekelo ‘Mzee wa Upako’ baada ya kudaiwa kumfanyia fujo jirani yake ameendelea kujibu madai hayo kwa mtindo wa ‘kudonoa donoa’ na jana aliwataka wanaodai kuwa alilewa siku hiyo wataje alikunywa pombe gani na katika baa gani. 

Wiki mbili zilizopita, taarifa kwenye vyombo vya habari zilisema kwamba Mchungaji Lusekelo alikwaruzana na majirani zake huku akidaiwa kuwa alikuwa amelewa jambo ambalo lilifanya achukuliwe na kuhojiwa na polisi. 

Lakini, tangu kuibuka kwa tukio hilo alikataa kulitolea ufafanuzi licha ya kutafutwa na vyombo vya habari, hata pale alipohudhuria ibada kanisani kwake aliwaambia waumini wake hatalizungumzia na badala yake alidonoadonoa baadhi ya matukio. 

Alipokwenda kanisa kwake kwa mara ya kwanza Novemba 25, Mchungaji Lusekelo alisema; “Kuna kitu nilikuwa nataka nikiseme, lakini sitakisema ili waendelee kusema haohao waliokuwa wanasema.Wakawaulize wenyewe. Nimeyaona magazeti hapa, ooh Mzee wa Upako, ooh Mzee wa Upako, sisemi. Sasa leo yupo hapa, na kwa taarifa yao watashindana sana, lakini hawatashinda. Hii ni kama kumpiga chura teke.”

Lakini, Novemba 28, Mchungaji huyo akajibu baadhi ya hoja akisema kwanza, maneno aliyotumia ambayo ni mshenzi, mpumbavu na mjinga siyo matusi kwani yameandikwa kwenye Biblia. Pili, watu hao ndiyo walianza kumtukana yeye baada ya kuwauliza wanatafuta nini eneo la getini kwake.

 Hoja nyingine alisema watu hao hawakuwa jirani zake kama inavyodaiwa kwani mtaani kwake wanaishi kama majambazi kutokana na mazingira ya kutofahamiana. 

Jana, Mchungaji Lusekelo akiwahubiria waumini wake alidonoa tena eneo jingine linalohusiana na tukio hilo, kwamba wanaodai alikuwa amelewa pombe, waeleze alikunywa pombe gani na baa gani. 

Akikaribishwa kwa wimbo wa kuabudu uitwao, ‘Nina haja nawe’ kabla ya kuanza kumtunza kwa sadaka, Mchungaji Lusekelo alisema watu wanaotuhumu kuwa alilewa, wanatakiwa kueleza alikunywa pombe gani na alikunywa akiwa eneo gani. 

“Wiki iliyopita nilikuwa Wizara ya Mambo ya Ndani, baadhi ya maofisa wakaniona , wewe Mzee wa Upako… Mzee wa Upako, askari mmoja akaniuliza wewe Mzee wa Upako unachukua sadaka halafu unaenda kunywa pombe. Nikawauliza, hiyo pombe nilikunywa wapi, halafu pombe zipo za aina nyingi, taja ni pombe gani, ukienda mbali zaidi ungeuliza nililewa nini, maana hata upako wa roho mtakatifu ni ulevi,” alisema. 

“Lakini kuna majina ya watu, mitaani inaitwa pombe, sasa sijui ni pombe gani hiyo….watashindana sana. Lakini kushindana siyo tatizo, je, mtashinda? Eti oooh hayo maneno tu hata kwenye kanga yapo, subiri tusiandikie mate na wino upo, ukitaka kummaliza Mzee wa Upako we mpige risasi tu,” alisema huku akishangiliwa na waumini wake.

 Alisema hakuna mwanadamu atakayeweza kumwangusha kwa kipawa na kalama Mungu aliyompatia. 

“Ndiyo maana unapojiita mtume leo unakuwa unajirusha kwenye harakati ambazo zilijengwa na baba zetu, ndiyo maana kumshinda shetani ni lazima, kuna mfumo umejengwa na mfumo huu uko imara kama chuma cha pua,” alisema. 

Katika ibada ya wiki iliyopita, mchungaji huyo alisema taarifa zinazosambazwa kumchafua hazitamvunja moyo wa kuendelea kufanya kazi ya uchungaji, huku akihoji kwanini magazeti yanaandika mabaya pekee na hayaandiki habari za uponyaji anaofanya kanisani kwake.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527