MWANAFUNZI WA DARASA LA 5 AJINYONGA


Mwanafunzi wa darasa la tano katika Shule ya Msingi Kizota mjiniDodoma, Yasin Abdallah (13) amekutwa amejinyonga bafuni nyumbani kwao baada ya kuchukizwa kufanya vibaya kwenye masomo yake. 

Kaimu Kamanda wa Polisi Mkoa wa Dodoma, Ernest Kimoli alisema tukio hilo lilitokea Desemba 2 eneo la Kizota Relini Manispaa ya Dodoma. 

Kimoli alisema baba mzazi wa mtoto huyo, Hassan Juma (53) aligundua kujinyonga kwa mwanaye saa 6:00 mchana.

“Sababu ya kujinyonga ni kuchukizwa na matokeo ya mitihani yake,”alisema. 

Diwani wa Kizota, Jamary Ngalya alisema mtoto huyo ambaye alizikwa juzi jioni, alianza kwa kuwaeleza wanafunzi wenzake Ijumaa kuwa atajinyonga. 

Alisema baada ya kutamka maneno hayo, wenzake walimwambia wanakwenda kumweleza mwalimu. Hata hivyo, baada ya kuwasikia wenzake aliwaambia kuwa anatania hawezi kufanya hivyo. 

Mwalimu Mkuu wa Shule ya Kizota, Juma Malecela alisema mwanafunzi huyo alihamia Oktoba kutoka mkoani Kigoma. 

“Katika matokeo ya kumaliza darasa la nne alikuwa wa 129 kati ya 132, inawezekana huko alikuwa anafanya vizuri,” alisema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527