MGANGA WA KIENYEJI AUAWA AKIMBAKA MGONJWA WAKE SHINYANGA


Kamanda wa jeshi jeshi la polisi mkoa wa Shinyanga ACP Muliro Jumanne akionesha vifaa vya uganga vya waganga wa kienyeji 22 waliokamatwa wakidaiwa kujihusisha na upigaji ramli chonganishi hivi karibuni-Picha kutoka maktaba ya Malunde1 blog 


****** 
Wananchi wenye hasira kali wamemuua mganga wa kienyeji aliyejulikana kwa jina la Kashinje Kashinje(55), mkazi wa kijiji cha Singita kata ya Usanda wilayani Shinyanga kwa kumshambulia kwa silaha za jadi wakati akijaribu kumbaka mwanamke mwenye umri wa miaka 20 (jina linahifadhiwa) aliyefika nyumbani kwa mganga huyo kupata tiba ili apate mtoto.

Kwa mujibu wa kamanda wa polisi mkoa wa Shinyanga ACP Muliro Jumanne Muliro tukio hilo limetokea Novemba 29 mwaka huu majira ya saa tano asubuhi.

Kamanda Muliro alisema mganga wa kienyeji Kashinje Kashinje alifariki dunia alipokuwa njiani akipelekwa hospitali baada ya kujeruhiwa kwa kitu chenye ncha kali jicho la kulia ma kupigwa kwa fimbo mgongoni na watu waliojichukulia sheria mkononi.

“Watu hao walijichukulia sheria mkononi baada mganga huyo kujaribu kumbaka mwanamke (jina linahifadhiwa) mkazi wa kijiji cha Ishinabulandi wilaya ya Shinyanga ambaye alikuwa akimtibu kwa tiba za asili ili aweze kupata mtoto”,alieleza kamanda Muliro.

Alisema tatizo lililompeleka mwanamke huyo kwa mganga ni kupata tiba ili aweze kupata mtoto.

Kamanda Muliro alibainisha kuwa chanzo cha tukio hilo ni tamaa za kimwili na uongo wa kimatibabu wa kutaka kumuingilia kimwili mgonjwa wake baada ya kumlewesha kwa dawa za kienyeji.

Aliongeza kuwa kutokana na kitendo hicho cha mganga wa kienyeji,mwanamke huyo alipiga kelele za kuomba msaada ndipo wananchi walifika na kuanza kumshambulia mganga huyo na kumsababishia maumivu makali yalisababisha chanzo cha kifo chake.

Kamanda Muliro alisema watu wawili wanaohojiwa kuhusiana na tukio hilo ambao ni Masaganya Katambi (45) na Shija Sele (40). 

Na Kadama Malunde-Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527