UKWELI KUHUSU KUFUFUKA KWA MSANII WA NYIMBO ZA ASILI NYANDA MADIRISHA 'THE SUPER STAR"



Msanii Nyanda Madirisha "The Super Star" enzi za uhai wake



Nyanda Madirisha enzi za uhai wake


Mwili wa Nyanda Madirisha ukiwa chini baada ya kupata ajali ya pikipiki na kufariki dunia huko Maswa mkoani Simiyu Agosti 06,2016


Pikipiki iliyosababisha kifo cha msanii Nyanda Madirisha tarehe 06.08.2016


Waombolezaji wakiwa wabeba jeneza lililobeba mwili wa Nyanda Madirisha tarehe 07.08.2016

Mazishi ya Nyanda Madirisha tarehe 07.08.2016


Nyanda Nchaina,ambaye sasa ni mrithi wa Nyanda Madirisha


Nyanda Nchaina,ambaye sasa ni mrithi wa Nyanda Madirisha
*******
Kumekuwepo taarifa zinazosambaa kwa kasi kuwa Msanii wa nyimbo za asili Nyanda Madirisha aliyefariki dunia Agosti 06,2016 akijiandaa kufanya show huko Maswa mkoani Simiyu kuwa  ameonekana akiwa hai “amefufuka” akipata matibabu kwa mganga wake wa kienyeji.Mwandishi mkuu wa Malunde1 blog Kadama Malunde,anaripoti.

Taarifa hizo zimeibua hisia tofauti tofauti kwa wapenzi wa nyimbo za asili hasa mashabiki wa Msanii Nyanda Madirisha "The Super star".

Kutokana na usumbufu mkubwa tumekuwa tukiupata hata sisi Malunde1 blog ikiwemo kupigiwa makumi ya simu kila kukicha,tukiwa wadau wakubwa wa nyimbo za asili tumeamua kuitafuta familia ya Nyanda Madirisha ili kupata ukweli wa kile kinachovumishwa kuwa msanii huyo amefufuka.

Leo Jumamosi Oktoba 22,2016 Malunde1 blog imezungumza na mdogo wake na marehemu anayejulikana kwa jina la “Nyanda Nchaina” ambaye ndiyo amerithi mikoba ya kaka yake Nyanda Madirisha katika usanii baada ya ukoo wao kukubaliana kuwa kijana Nyanda Nchaina amrithi kaka yake.

Nchaina ameeleza kusikitishwa na taarifa hizo na kusema kuwa siyo za kweli bali ni uzushi tu ulionezwa na baadhi ya watu wachache walioamua kujirekodi na kudai kuwa Nyanda Madirisha ameokana na ataendelea kuimba.



“Hizo taarifa sisi kama familia tumezipata na kuzifuatilia na kujua chanzo kuwa kuna kikundi cha watatu ambao wamejirekodi sauti na kuisambaza mtandaoni,mwingine kajiita Nchaina,mwingine Kajipa jina la Nyanda Madirisha na mwingine katumia jina la mtangazaji wa Kahama fm,kwamba huyo mtangazaji ndiyo anafanya mahojiano nao,Nyanda Madirisha anaeleza kuwa hajafa ataendelea kuimba”,amesema Nchaina.

“Wamejirekodi sauti kuutangazia umma kuwa Nyanda Madirisha yuko hai,huu ni upotoshaji wa hali ya juu,ambao umetufedhesha wanafamilia na watu wote wenye mapenzi mema na Nyanda Madirisha,tunaomba waliokuwa mashabiki wa Nyanda Madirisha na wapenzi wote wa nyimbo za asili kupuuza taarifa hizo,ndugu yetu hatuko naye katangulia mbele za haki”,ameeleza Nchaina.

Amesema hawana uhakika na taarifa za kufufuka kwa Nyanda Madirisha na kwamba kuendelea kueneza taarifa kuwa ndugu yao kaonekana kunawafanya wakose amani na wakati mwingine kushindwa kufanya kazi za kila siku kutokana na kuwakumbusha machungu ya kupoteza ndugu yao.

Akizungumzia kuhusu jinsi kifo cha kaka yake kilivyotokea,Nyanda Nchaina ambaye sasa ndiyo anafanya kazi ya usanii wa ndugu yake baada ya ukoo wao kumtaka arithi kazi ya kaka yake anasema Nyanda Madirisha alifariki kwa ajali ya pikipiki na hakuwa na majeraha yoyote.

“Nyanda Madirisha alikuwa anaishi Kahama,lakini alizikwa Mbogwe mkoani Geita kwa baba yake Agosti 07,2016 ,alifariki kwa ajali ya pikipiki Agost 6,2016 wakati akitoka kufuata mafuta kwa ajili ya gari lake la matangazo ili kwenda uwanjani kuendelea na show Shinyanga Mwenge wilayani Maswa mkoani Simiyu”,ameeleza Nchaina. 

"Baada ya kufanya mazishi,ndugu walikubaliana kuwa usanii wa Nyanda Madirisha uchukuliwe na mdogo wake na marehemu Nchaina "ambaye bi mimi,ili kuifanya bendi iendelee badala ya kupotea baada ya Nyanda Madirisha kufariki..sasa nafanya kazi aliyokuwa anafanya kaka yangu,nimerithi kazi zake,nimerithi kundi lake la muziki/wachezaji,vifaa vya muziki na vitu vingine",ameongeza Nchaina.
SIKILIZA SAUTI HAPA CHINI,NYANDA NCHAINA AKIZUNGUMZA NA MALUNDE1 BLOG KUHUSU TAARIFA ZA KUFUFUKA KWA NYANDA MADIRISHA


TAZAMA HAPA VIDEO YA WIMBO WA NYANDA MADIRISHA ALIOJITABIRIA KIFO

VIDEO YA MAZISHI YA NYANDA MADIRISHA


WIMBO MPYA WA NYANDA NCHAINA "MRITHI WA NYANDA MADIRISHA

TAZAMA HAPA CHINI VIDEO YA NCHAINA Ft MALIGANYA KUHUSU KIFO CHA NYANDA MADIRISHA

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527