HATMA YA KESI YA BOSI WA JAMIIFORUMS MEI 28



Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imepanga Mei 28, 2018 kutoa uamuzi kama Mkurugenzi Mtendaji wa Mtandao wa Jamii Forums, Maxence Melo na mwenzake wana kesi ya kujibu au la.

Uamuzi huo wa Mahakama umetolewa leo Mei 22, 2018 na Hakimu Mkazi Mwandamizi wa Mahakama hiyo, Godfrey Mwambapa baada ya upande wa mashtaka kufunga ushahidi wao.

Katika kesi hiyo ya jinai namba 457/2016, Melo na mwanahisa wa mtandao huo, Micke William wanakabiliwa na shtaka la kushindwa kutoka ushurikiano kwa Jeshi la Polisi kwa kuzuia taarifa binafsi za wateja wao.

Awali, Wakili wa Serikali, Batilda Mushi amedai mahakamani hapo kuwa kesi hiyo imekuja kwa ajili ya uamuzi.

Baada ya maelezo hayo, Hakimu Mwambapa ameahirisha kesi hiyo hadi, Mei 28 atakapotoa uamuzi dhidi ya Mello na mwenzake kama wanakesi ya kujibu au laa.

Tayari mashahidi wawili wa upande wa Jamhuri wameshatoa ushahidi wao mahakamani hapo dhidi ya washtakiwa.

Katika kesi ya msingi, Micke na Melo, wanadaiwa kuwa kati ya Mei 10 na Desemba 13,2016 , kwenye eneo la Mikocheni, wakiwa Wakurugenzi wa Mtandao wa Jamii Media Co Ltd ambao unaendesha tovuti ya Jamii Forums wakijua Jeshi la Polisi Tanzania linafanya uchunguzi kuhusiana na mawasiliano ya kimtandao yaliyochapishwa katika tovuti yao kwa njia ya kuzuia uchunguzi huo, walishindwa kutekeleza amri ya kutoa data walizonazo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527