TRA SHINYANGA YAZINDUA KAMPENI YA TUWAJIBIKE "UKIUZA TOA RISITI, UKINUNUA DAI RISITI"


Na Kadama Malunde - Malunde 1 blog

Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga imezindua Kampeni ya TUWAJIBIKE inayolenga kuwakumbusha na kuwahimiza wafanyabiashara kuwajibika katika kutoa risiti halali za EFD wanapouza bidhaa au huduma na wanunuzi/wateja wa wafanyabiashara kuhakikisha wanapata risiti sahihi.

Uzinduzi wa Kampeni ya Tuwajibike ulioenda sanjari na ukaguzi wa risiti kwa wafanyabiashara na wanunuzi wa bidhaa umefanyika leo Mei 11,2023 Mjini Shinyanga ambapo TRA Mkoa wa Shinyanga imekutana na wafanyabiashara na wateja wa wafanyabiashara na kuwasisitiza umuhimu wa utoaji risiti na kudai risiti.


Akizungumza wakati wa uzinduzi wa Kampeni ya Tuwajibike katika mkoa wa Shinyanga, Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga, Faustine Cosmas Mdessa amesema Kampeni ya Tuwajibike ni Kampeni ambayo imeanzishwa na TRA na kuzinduliwa rasmi kitaifa Mei 3,2023 na itakuwa endelevu na imepangwa kutekelezwa kote nchini kwa kushirikiana na wadau mbalimbali wa TRA.

“Kampeni ya Tuwajibike ina malengo makuu mawili ambayo ni kuwakumbusha na kuwahimiza wafanyabiashara kuwajibika katika suala ya utoaji wa risiti halali za EFD kwa kila bidhaa wanazouza na huduma wanazozitoa lakini pia inawakumbusha na kuwahamasisha wanunuzi ambao ni wateja wa wafanyabiashara kuwajibika kwa kuhakikisha wanadai risiti halali za EFD pamoja na kuzikagua ili kujiridhisha kuwa risiti hiyo inakidhi vigezo vyote muhimu vya risiti halali ya EFD ili pesa wanazolipa na risiti iwe sahihi kwa kiwango walicholipa”,amesema Mdessa.

Amevitaja vigezo vikuu vinavyoonesha kuwa risiti halali ya EFD ni jina la muuzaji,tarehe na muda halisi ya mauzo, kiasi/gharama halisi ya pesa iliyonunuliwa bidhaa au huduma pamoja na TIN na jina la mnunuzi.

Amefafanua kuwa TRA imeamua kuhimiza na kusimamia suala la wafanyabiashara kutoa risiti sahihi wanapouza bidhaa au kutoa huduma na wanunuzi kudai risiti kwa malipo halali waliyoyafanya hali ambayo itasaidia sana katika kuhakikisha mapato ya serikali kuu yanafika katika mfuko sahihi.
Maafisa kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga wakikagua risiti ya bidhaa alizokutwa nazo mwananchi aliyekuwa anasafirisha magodoro ambapo mwananchi huyo alikutwa na risiti halali ya bidhaa alizopewa kuzisafirisha.

“Kumetokea kawaida ya aidha wafanyabiashara kutoa risiti pungufu au kutotoa risiti kabisa na wanunuzi kutodai risti hii inamaanisha kwamba uwezekano mkubwa wa pesa ya serikali kutofika kule inakoelekea”,amesema Mdessa.


“Kampeni ya Tuwajibike inahusu biashara na huduma zote hivyo itahusisha biashara zote nchini ila mkazo zaidi utawekwa katika maeneo korofi zaidi katika utoaji wa risiti za EFD kama vile eneo la usafirishaji wa vifurushi au vipeto vinavyokwenda mikoani kwa usafiri wa mabasi. Eneo jingine ni kumbi za starehe ikiwemo baa na kumbi za muziki. Ukinywa bia au soda dai risiti”,amesisitiza Meneja huyo wa TRA Mkoa wa Shinyanga.


Amesema hatua za kisheria zitakazochukuliwa kwa mujibu wa sheria ya adhabu ya makosa katika matumizi ya mashine za EFD ambapo mfanyabiashara atayebainika kutokutoa risiti halali ya EFD au kufanya udanganyifu wowote ule atatozwa faini ya kuanzia shilingi 3,000,000/= hadi shilingi 4,500,000/= au kifungo kisichozidi miaka mitatu jela au vyote kwa pamoja.


“Kwa mnunuzi atakayebainika kufanya manunuzi bila ya kudai risiti halali ya EFD atatozwa faini ya kuanzia shilingi 30,000/= hadi shilingi 1,500,000/=”,amesema Mdessa.


“Ombi langu kwa watanzania kwa lengo la tuwajibike, kitu ambacho ni endelevu tunawashauri kwa kila anayefanya biashara ahakikishe anatoa risiti na kama kuna tatizo lolote awasiliane na TRA haraka iwezekanavyo na mnunuzi ahakikishe anadai risiti kwa malipo sahihi aliyofanya ili kuepuka adhabu inayoweza kuipata kwa kutodai risiti”,amesema.

"Tunapenda kutoa wito kwa wafanyabiashara wote kuwajibika kwa kutoa risiti halali za EFD bila ya kushurutishwa na wanunuzi kudai risiti halali za EFD kwa kila manunuzi watakayofanya ili kuepuka usumbufu usio wa lazima na wakati huo huo kuisaidia serikali kutimiza malengo yake kuwaletea wananchi maendeleo na kukuza uchumi wan chi yetu. Tuwajibike!”, ameongeza Mdessa.
Kwa upande wake, Meneja Msaidizi Upande wa Madeni TRA Mkoa wa Shinyanga, Estomih Mossi amesema njia inayotumika kuendesha kampeni ya Tuwajibike ni pamoja na kufuatilia utoaji risiti halali za EFD nchi nzima na kuchukua hatua kwa wauzaji wasiofuata sheria katika utoaji wa risiti halali za EFD kama vile kutokutoa risiti ya EFD, kutoa risiti yenye mapungufu, kutumia risiti moja ya kushinikiza mizigo kadhaa, kufanya biashara ya kuuza risiti pasipokuwa kwa watu wengine ambao hawana mashine za EFD na mnunuzi kutokudai risiti baada ya kununua bidhaa au huduma.


Nao baadhi ya Wafanyabiashara akiwemo Adonikamu Kweka na Manka Geofrey Mushi wamesema hivi sasa kuna mwamko mkubwa kwa wafanyabiasha kutumia mashine za EFD huku wakieleza kuwa utoaji risiti pia unasaidia sana katika kutunza kumbukumbu za mauzo.


Kwa upande wao wanunuzi wa bidhaa akiwemo Moyo Bunzali na Khamis Kasole wamesema pindi mfanyabiashara anapotoa risiti na mnunuzi kudai risiti inasaidia katika kukusanya kodi za serikali kwa halali na kwamba ukikwepa risiti maana yake unaiibia serikali.

Wasiliana na Kituo cha Huduma kwa MlipaKodi kwa namba za bure 0800 750 075 au 0800 780 078 au 0800 110 016 . Pia anaweza kutumia ujumbe kwa njia ya WhatsApp namba 0744 233 333 au kutumia barua pepe kwenda huduma@tra.go.tz au kwenye mitandao ya kijamii.

ANGALIA PICHA HAPA CHINI
Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga, Faustine Cosmas Mdessa akielezea kuhusu Kampeni ya Tuwajibike inayoendeshwa na TRA inayolenga kuwakumbusha na kuwahimiza wafanyabiashara kuwajibika katika kutoa risti halali za EFD na wateja wa wafanyabiashara kuhakikisha wanapata risiti sahihi. Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog
Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga, Faustine Cosmas Mdessa akielezea kuhusu Kampeni ya Tuwajibike inayoendeshwa na TRA inayolenga kuwakumbusha na kuwahimiza wafanyabiashara kuwajibika katika kutoa risti halali za EFD na wateja wa wafanyabiashara kuhakikisha wanapata risiti sahihi.
Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga, Faustine Cosmas Mdessa akielezea kuhusu Kampeni ya Tuwajibike inayoendeshwa na TRA inayolenga kuwakumbusha na kuwahimiza wafanyabiashara kuwajibika katika kutoa risti halali za EFD na wateja wa wafanyabiashara kuhakikisha wanapata risiti sahihi.
Meneja wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga, Faustine Cosmas Mdessa akielezea kuhusu Kampeni ya Tuwajibike inayoendeshwa na TRA inayolenga kuwakumbusha na kuwahimiza wafanyabiashara kuwajibika katika kutoa risti halali za EFD na wateja wa wafanyabiashara kuhakikisha wanapata risiti sahihi.
Maafisa kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga wakikagua risiti ya bidhaa alizokutwa nazo mwananchi aliyekuwa anasafirisha magodoro ambapo mwananchi huyo alikutwa na risiti halali ya bidhaa alizopewa kuzisafirisha.
Msafirishaji mizigo akielezea umuhimu wa kudai risiti wakati wa kununua bidhaa wakati maafisa kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga walipomsimamisha kukagua kama ana risiti ya bidhaa alizonunua ambapo mwananchi huyo alikutwa na risiti ya bidhaa alizopewa kuzisafirisha
Meneja Msaidizi Upande wa Madeni TRA Mkoa wa Shinyanga, Estomih Mossi akizungumza wakati wa ukaguzi wa risiti kwa wafanyabiashara na wanunuzi wa bidhaa Mjini Shinyanga
Maafisa kutoka Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Shinyanga wakiwa kwenye duka la mfanyabiashara Adonikamu Kweka wakati wakiendelea kukagua risiti za bidhaa
Mfanyabiashara Adonikamu Kweka (kulia) akionesha risiti ya bidhaa alizouza. Kushoto ni Meneja Msaidizi Upande wa Madeni TRA Mkoa wa Shinyanga, Estomih Mossi
Mfanyabiashara Adonikamu Kweka akielezea umuhimu wa kutoa risiti
Maafisa wa TRA wakiondoka kwenye duka la Mfanyabiashara Adonikamu Kweka
Mfanyabiashara Manka Mushi akielezea umuhimu wa kutoa risiti
Mnunuzi wa bidhaa Moyo Bunzali  akielezea umuhimu wa kudai risiti
Waafisa wa TRA wakiwa katika duka la Mfanyabiashara Emmanuel Lazaro
Mnunuzi wa bidhaa Khamis Kasole akielezea umuhimu wa kudai risiti
Bango likiwa nje ya Kumbi ya Starehe maarufu  The Dees's Lounge Mjini Shinyanga inayohamasisha kudai risiti
Maafisa wa TRA wakikagua risiti katika Kumbi ya Starehe maarufu  The Dees's Lounge Mjini Shinyanga 
Maafisa wa TRA wakikagua risiti katika Kumbi ya Starehe maarufu  The Dees's Lounge Mjini Shinyanga 
Maafisa wa TRA wakikagua risiti katika Kumbi ya Starehe maarufu  The Robi's Bar & Grill Mjini Shinyanga 
Maafisa wa TRA wakikagua risiti katika Kumbi ya Starehe maarufu  The Robi's Bar & Grill Mjini Shinyanga.

Picha na Kadama Malunde - Malunde 1 blog


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

1/Post a Comment/Comments

  1. Naunga mkono hoja na dhima ya TRA shy kwa kutuhimiza cc wafanyabiashara kutoa risiti kwani RISITI NI SHAHIDI WA KWELI KWETU NA WATEJA WETU🙏

    ReplyDelete

Post a Comment