HAKIMU AWASHANGAA POLISI KUTOMSHIKA ANAYEDAIWA KUUA


HAKIMU wa Mahakama ya Wilaya ya Arumeru, Patricia Kisinda amewashangaa Polisi kutomkamata Felix Mmasi (41) anayedaiwa kuua bila kukusudia licha ya kuagiza akamatwe.

Pia ameshangazwa na Polisi kuileta tena kesi hiyohiyo namba 17/2017 mahakamani hapo kwa kosa hilohilo la kuua bila kukusudia.

Kisinda aliyasema hayo baada ya washitakiwa Michael Laizer (35) na Lucas Mmasi (35) wote kushitakiwa kwa mauaji ya JuliusTarangire.

Awali Wakili wa Serikali, Neema Joseph alidai mahakamani hapo washitakiwa hao Machi 28, 2015 Nadosoito Arusha walimuua Julius.

Alidai kesi hiyo ilifika mahakamani hapo kwa mara ya kwanza Aprili 15, 2015, walikana kosa hilo na kesi hiyo kuahirishwa kusubiri ipelekwe Mahakama Kuu kusikilizwa.

Lakini Wakili huyo alidai inashangaza kuona tena katika mauaji hayohayo mshitakiwa kwenye kesi namba 14/2015 ambaye ni Felix anafikishwa mahakamani kwa mara ya kwanza kwa kosa hilohilo na kuachiwa kwa dhamana.

Alidai Felix alisomewa mashitaka Aprili 10, 2015 na ikadaiwa kuwa Machi 28, 2015 alimuua Tarangire bila kukusudia Nadosoito, Arumeru.

Baada ya kusomewa mashitaka, Felix alipewa dhamana lakini haijulikani jinsi dhamana yake ilivyotoka na baada ya muda Mahakama ilitoa notisi ya kukamatwa kwake na hadi leo hajafika mahakamani hapo wala wadhamini wake.

Kutokana na sintofahamu hiyo, Hakimu Kisinda alisema mazingira ya kesi hiyo yana utata na kuhoji ni kwa nini Polisi wanasita kumkamata Felix ili afike kujibu tuhuma zinazomkabili. Kesi hiyo imeahirishwa hadi Machi 26, 2018.

IMEANDIKWA NA VERONICA MHETA - HABARILE ARUSHA

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527