MAHAKAMA ya Hakimu Mkazi Mfawidhi Wilaya ya Dodoma imwamuru Mkuu wa Gereza la Isanga, ampeleke mshitakiwa Tito Onesmo Machibya 'Nabii Tito' akapimwe afya ya akili kama korti ilivyoagiza.
Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mahakama hiyo, James Kareyemaha jana amemuagiza mkuu huyo wa gereza ampeleke Tito katika Taasisi ya Magonjwa ya Akili Isanga ili mahakama iendelee na shauri hilo.
Awali, wakili wa Serikali, Beatrice Nsana aliiambia mahakama hiyo kuwa kesi hiyo imekuja kusikilizwa ndipo Hakimu Kayeremaha alipohoji vielelezo vilivyotakiwa kuwasilishwa mahakamani hapo.
Mshitakiwa Tito ameieleza mahakama hiyo kuwa bado hajapelekwa kufanyiwa vipimo kama ilivyoagizwa, hivyo mahakama imeamuru jambo hilo kutekelezwa.
Kesi hiyo imeahirishwa hadi Machi 5, mwaka huu, kwa ajili ya kusikilizwa tena.