Na Dotto Kwilasa,DODOMA
Serikali imeeleza kuwa mafanikio ya Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050 yanategemea kwa kiasi kikubwa kuimarishwa kwa sekta ya kilimo, huku Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) ikiagizwa kuelekeza nguvu zaidi katika maeneo ya kimkakati yatakayoongeza uzalishaji na kuinua maisha ya Watanzania.
Waziri wa Fedha, Khamis Mussa Omar, alitoa agizo hilo baada ya kutembelea banda la TADB katika Maonesho ya 33 ya Kitaifa na Kimataifa ya Nane Nane yanayoendelea katika Viwanja vya Dkt. John Samuel Malecela, Nzuguni jijini Dodoma.
Amesema uwekezaji katika kilimo, mifugo, uvuvi na misitu ni nguzo muhimu ya kufikia malengo ya muda mrefu ya Taifa, ikiwemo azma ya kuwa na uchumi wa dola za Marekani trilioni moja ifikapo utekelezaji wa Dira hiyo.
Waziri Omar alisema kuongezeka kwa uwezo wa kifedha wa TADB kunapaswa kwenda sambamba na uwekezaji wenye tija utakaowanufaisha wakulima na wadau wengine katika mnyororo mzima wa thamani wa kilimo.
TADB, ambayo mtaji wake umeongezeka kutoka shilingi bilioni 60 hadi zaidi ya shilingi bilioni 400 kutokana na uwekezaji wa Serikali, ndiyo mdhamini mkuu wa maonesho hayo yenye kaulimbiu “Tambua Soko, Ongeza Uzalishaji, Timiza Dira ya Taifa ya Maendeleo 2050.”




Social Plugin