WAOMBOLEZAJI WA KULIPWA WAZUA VURUGU MSIBANI...MFIWA AJIFICHA MSALANI


Picha ya maktaba kundi la vijana wakibishana kando ya jeneza
***
Sinema ya bwerere imetokea eneo la Lugari, Kakamega nchini Kenya baada ya vijana waliolipwa kuomboleza kuzua fujo kwa mwenyeji wao alipowaandalia sima kwa kuku badala ya kuwalipa pesa. 

Wapambe hao ambao jukumu lao ni kunogesha mazishi kwa densi maalum, nyimbo na shamrashamra za aina yake walidai mwenyeji wao aliwatapeli badala ya kutekelea wajibu waliokubaliana.

“Huu ni uhuni! Twanfanyiwa uhuni mchana peupe na hatung’atuki hapa hadi tupewe haki yetu,” mmoja wao alisikia akidai kulingana na ripti ya Taifa Leo.

 “Ni kweli huyu ni tapeli mkubwa. Hajatimiza hata moja tuliloafikiana,”wa pili alieleza. 

“Anafikiri kuruka ruka tukicheza na sarakasi zote hizi ni kazi rahisi? Kazi ni kazi jamani,” kijana wa tatu naye aliongea.

Penyenye zinaarifu kwamba siku ya kisanga majamaa walijaajaa vyema kushirikiana na watu wa familia kwa mipango yote kwani donge waliloahidiwa lilikuwa nono.

Ulipofika wakati wa kutoa jeneza nje ya nyumba, walisakata ngoma kwa bidii huku wengine wakijiangusha kama majani wakiomboleza huku wakitiririkwa na machoni ungedhani ni wao waliofiwa.

 Inasemekana hata wakati jeneza lilipokuwa likiteremshwa kaburini mmoja wao alitishia kujirusha ndani lakini akadhibitiwa na kutulizwa jazba zake na wenzake.

 Baada ya mazishi kukamilika, waliketi kwenye hema maalum na kula chakula cha yapata watu hamsini lakini baada ya kumaliza na kuanza kudai malipo hapo ndipo maneno yalianza kwenda mrama.

 “Sijawahi kuona watu wenye hamu ya kula kama nyinyi. Mwajua mmekula robo ya chakula kilichopikwa?” mama mwenye aliwaulia mabarobaro.

“Usilete upumbavu hapa. Tujuavyo chakula ni cha kila mmoja aliyehudhuria. Tulipe pesa zetu na uwache upumbavu,” walidai.

 Inasemekana kuwa mwenyeji alipokataa kuwalipa majamaa, kivumbi kikazuka ghafla. Vijana hao walianza kutupa mawe, kurusha viti kila mahali na watu kuumizwa.

 Mwenyeji alipoona mambo yamekuwa mabaya aliamua kujifungia msalani. 

“Toka! Toka humo ndani wewe tapeli mkubwa. Leo utajua utapeli una mwisho,” mkubwa wa vijana hao aliwaka.

 Penyenye zinasema mama alipohisi maisha yake yamo hatarini aliamua kubadili msimamo na kutoka mafichoni.

Mama huyo ambaye alijulikana kuwa mkono wa birika alilazimika kuwalipia vija hao mara dufu ya pesa walizokuwa wameahidiana.

 Hadi leo mama anasikitika kukadiria hasara aliyosababisha kutokana na tamaa yake.

CHANZO - TUKO NEWS


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments