ATIWA MBARONI KWA TUHUMA YA KUSAFIRISHA SHEHENA YA DAWA ZA BINADAMU


Jeshi la Polisi Mkoani Dodoma linamshikilia Fredrick Anaclet Maxmilian (38) mkazi wa Mbagala Jijini Dar es Salaam kwa tuhuma ya kusafirisha shehena ya madawa ya binadamu sampuli 149 baadhi yakiwa na nembo ya MSD.


Hayo yamebainishwa leo na Kamanda wa Jeshi la Polisi Mkoa wa Dodoma, SACP. Gilles Muroto wakati akizungumza na waandishi wa Habari leo Jijini Dodoma.

Aidha Muroto amesema kuwa mtuhumiwa huyo alikamatwa mnamo tarehe 09/07/2020 majira ya saa moja jioni.

Amesema katika mahojiano na mtuhumiwa huyo imeonekana kuwa yeye siyo daktari wala mfamasia na dawa ila anashirikiana na mfamasia ambaye ni mtumishi wa Serikali (jina limehifadhiwa) huko mkoani Tabora.

Kamanda Murotto amesema uchunguzi unaendelea na watuhumiwa watafikishwa mahakamani.

Kwa upande wake Kaimu Mganga Mkuu wa Hoapitali ya mkoa wa Dodoma Dkt.Samuel Seseja amesema shehena hiyo ina dawa aina nane ambapo zipo zenye nembo ya Serikali,pia zipo zenye nembo ya MSD na nyingine hazina nembo.

Hata hivyo amesema dawa hizo hazitakiwi kuuzwa na mtu yeyote kwani kuna wazabuni wa kufanya kazi hiyo katika kila mkoa.

Lengo lilikuwa ni kuziuza kwenye maduka mbalimbali ya dawa jambo ambalo siyo sahihi.

“Uuzaji wa dawa unalindwa na sheria inayotoa namna gani dawa hizo ziweze kununuliwa na kuuzwa, hivyo hicho ni kinyume na sheria inayosimamia suala la dawa na vifaa tiba.”amesema Dkt.Seseja.

Alitumia fursa hiyo kutoa wito kwa wafanyabiashara na watoa huduma kutojihusisha na ununuzi wa dawa kutoka kwa vyanzo ambavyo havifahamiki na kwamba  wanapaswa kununua kwenye maduka ya dawa yaliyosajiliwa na mfamasia Mkuu wa Serikali.

Pia amewataka kutojihusisha na watoa huduma wasio waaminifu wanaoitia doa Serikali inayofanya kazi nzuri ya kuwahudumia wananchi.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527