SHIRIKA LA THUBUTU AFRICA INITIATIVES, USAID TULONGE AFYA WAENDESHA TAMASHA LA AKINA MAMA WENYE WATOTO CHINI YA MIEZI 6



Kaimu Mganga Mkuu wa mkoa Shinyanga Dkt. Timoth Sosoma akizungumza wakati akifungua tamasha la akina mama wenye watoto wa chini ya miezi 6 katika Kata ya Chibe, Manispaa ya Shinyanga kwa lengo la kuhamasisha matumizi ya huduma za afya ili kupunguza vifo vya mama na mtoto mkoani Shinyanga leo Jumatano Julai 15,2020.

Kaimu Mganga Mkuu mkoa wa Shinyanga Dk. Timoth Sosoma akikabidhi zawadi za taulo za watoto kwa wazazi walioshiriki katika washa hiyo. Taulo hizo zimetolewa na shirika la Thubutu Africa Initiatives kwa kushirikiana na T-Marc Tanzania.
Afisa Mradi wa Tulonge Afya Emanuel Marunda kutoka shirika la Thubutu Africa Initiatives, akizungumza kwenye tamasha la akina mama wenye watoto wa chini ya miezi 6 katika Kata ya Chibe, Manispaa ya Shinyanga kwa lengo la kuhamasisha matumizi ya huduma za afya ili kupunguza vifo vya mama na mtoto mkoani Shinyanga leo Jumatano Julai 15,2020.
***

Na Stephen Kanyefu - Malunde 1 blog


Shirika lisilokuwa la kiserikali la Thubutu Africa Initiatives kwa kushirikiana na USAID Tulonge Afya wameendesha tamasha la akina mama 'Mother meet up' wenye watoto wa chini ya miezi 6 katika Kata ya Chibe, Manispaa ya Shinyanga kwa lengo la  kuhamasisha tabia za kiafya kwa kina mama ikiwa ni pamoja na unyonyeshaji wa maziwa ya mama pekee kwa miezi 6 ya mwanzo, matumizi ya njia za kisasa za afya ya uzazi ili kupishanisha watoto na matumizi sahihi ya vyandarua vyenye dawa ya muda mrefu ili kujikinga na malaria.

Tamasha hilo limefanyika leo Jumatano Julai 15, 2020 katika kata ya Chibe ambapo mgeni rasmi alikuwa Kaimu Mganga Mkuu wa mkoa wa Shinyanga Dkt. Timoth Sosoma ambapo miongoni mwa walioshiriki katika warsha hiyo ni pamoja na wazazi na walezi wenye watoto chini ya umri wa miezi 6, viongozi wa dini, kamati ya afya ya mkoa wa Shinyanga (RHMT) na kamati ya afya ya manispaa Shinyanga (CHMT).

Akifungua tamasha hilo, Kaimu Mganga Mkuu wa mkoa Shinyanga Dkt. Timoth Sosoma alisema  ili kuwa na jamii yenye afya ni vyema wazazi wakazingatia kanuni bora za afya ikiwa ni pamoja na kutumia vyandarua vyenye dawa na kuachana na dhana potofu ya kuwa vyandarua hivyo vina madhara.

“Wengine wanasema wanapoteza nguvu za kiume hilo jambo sio la kweli vyandarua vinawasaidia kupunguza adha pale anapokuwa mbu hamgusi wanalala usingizi wa moja kwa moja vyandarua vipo salama vimethibitishwa havina madhara na havipunguzi nguvu za kiume”,alisema.

“Jamii kwa sasa imeanza kuelewa matumizi wa kutumia vyandarua, tofauti na hapo awali walikuwa wanatumia kufugia kuku,vifaranga lakini kwa sasa matumuzi yapo juu na serikali bado inaendelea kuongeza nguvu katika upatikanaji wa vyandarua”,aliongeza Dkt. Sosoma


Naye Afisa Mradi wa USAID Tulonge Afya kutoka Shirika la Thubutu Africa Initiatives  Emanuel Marunda amesema:

"Tamasha hili ni sehemu ya utekelezaji wa Mradi wa USAID Tulonge Afya ambapo lengo la tamasha hili ni kuhamasisha tabia za kiafya kwa wamama wenye watoto chini ya miezi 6 ikiwemo kulala kwenye chandarua kilichowekwa dawa ya muda mrefu,  kutafuta Huduma za afya unapoona dalili za homa kwa watoto, Matumizi ya njia mbalimbali za afya ya uzazi ili kumpa mama nafasi ya kupumzika na mtoto kukua,  kunyonyesha maziwa ya mama pekee kwa miezi sita ya mwanzo".

Marunda alisema lengo kuu la mradi huo unaofadhiliwa na USAID kupitia shirika la fhi360 na T-Marc Tanzania ni kuhamasisha mabadiliko ya tabia za watu kiafya ikiwa ni pamoja na wajawazito kuhudhuria kliniki mapema na kujifungulia katika vituo vya kutolea huduma za afya ili kupunguza vifo vya uzazi, wazazi na walezi wa watoto chini ya miezi sita kutekeleza tabia za kiafya ili kupunguza vifo vya watoto wa chini ya miezi sita.

Alitaja malengo mengine kuwa ni kuhamasisha matumizi ya njia za kisasa za afya ya uzazi kwa wazazi ili kupishanisha watoto na kwa vijana ili kupunguza mimba za utotoni na vili vile kuhamasisha upimaji wa VVU na kuanza huduma za tiba na matunzo mapema kwa watu walio katika hatari ya kupata maambukizi ya VVU.

"Tunautekeleza mradi huu katika kata zote 17 za Manispaa ya Shinyanga na kata 26 za Halmashauri ya wilaya ya Shinyanga",alieleza Marunda.


Marunda aliwahamasisha akina mama hao kutumia huduma za afya ili kupunguza vifo vya mama na mtoto mkoani Shinyanga ikiwa ni pamoja na kufuata huduma haraka katika vituo vya kutolea huduma za afya endapo mtoto atakuwa na dalili za ugonjwa wowote.

Kwa upande wake Afisa Lishe Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga Joanitha Jovin alitaja sababu zinazochangia wazazi kukosa maziwa wakati wa kunyonyesha kuwa ni pamoja na mzazi kukosa muda wa kupumzika na kukosa lishe bora.

“Hayupo mwanamke yoyote aliyejifungua akakosa maziwa ya kunyonyesha, kinachosababisha mama kuwa na maziwa madogo ni kutotumia chakula chenye lishe, matunda, mboga za majani na maji hawanywi”,alisema Jovin.

“Ili maziwa yaweze kutoka kwa wingi akili inatakiwa kuwa imetulia msongo wa mawazo huchangia uzalishaji mdogo wa maziwa”, aliongeza.

Nao akina mama walioshiriki katika tamasha hilo  walishirikishana uzoefu wa malezi ya watoto ili kuhamasishana katika kutekeleza tabia za kiafya huku wakiahidi kuyatumia vyema mafunzo hayo kwa makuzi bora ya watoto wao.
Afisa lishe wa Manispaa ya Shinyanga Joanitha Jovin, akizungumza katika tamasha la akina mama wenye watoto wa chini ya miezi 6 katika Kata ya Chibe, Manispaa ya Shinyanga na kuwataka wazazi kuhakikisha wanawanyonyesha watoto wao kwa muda wa usiopungua miezi sita ili uwa na watoto wenye afya.
Mratibu wa Elimu ya Afya kwa Umma mkoa wa Shinyanga, Halima Hamis akiwasisitiza wazazi kutumia njia za uzazi wa mpango kwani ni salama na hazina madhara.
Zubeda Joseph Mayunga akichangia hoja kwenye tamasha la akina mama wenye watoto wa chini ya miezi 6 katika Kata ya Chibe, Manispaa ya Shinyanga.

Wazazi na walezi wakifanya kazi ya makundi ikiwa njia shirikishi iliyotumiwa kuhakikisha lengo washiriki wanakuwa na uelwa wa pamoja.
Washiriki wa tamasha la akina mama wenye watoto wa chini ya miezi 6 katika Kata ya Chibe, Manispaa ya Shinyanga  katika picha ya pamoja

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527