KATIBU TAWALA MKOA WA SIMIYU ATENGUA AGIZO LA MKUU WA WILAYA KUTAKA WATUMISHI WACHANGIE FEDHA KUNUNUA MASHINE YA ULTRA SOUND ILIYOIBIWA


Katibu Tawala Mkoa wa Simiyu, Jumanne Sagini ametengua agizo la Mkuu wa Wilaya ya Bariadi, Festo Kiswaga la kutaka Wafanyakazi wote wa Hospitali ya Wilaya hiyo,kuchangishwa fedha kulingana na kiwango cha mshahara ili kununua mashine mpya ya Ultra sound kufidia mashine iliyoibiwa.


“Kuchangisha watumishi wote sio sahihi, kuna wengine walikuwa likizo na watakuwa wanaingizwa kwenye tukio ambalo pengine hawahusiki, Serikali ina vyombo vya uchunguzi, na tukio hilo ni moja ya kazi yao, Polisi ianze uchunguzi akibainika anayehusika achukuliwe hatua"  Amesema Sagini


Katika kikao chake na watumishi wa hospitali hiyo kilichofanyika jana,  Mkuu huyo wa Wilaya  Festo Kiswaga alitoa siku saba kwa watumishi wote kuchanga kulingana na mishahara kwa kila mmoja kuhakikisha wananunua mashine hiyo.
 


Kiswaga alimtaka Mganga Mkuu wa Halmashuari hiyo na  Mkurugenzi wa Halmashuari kuhakikisha ikifika Agosti 21, wapeleke mashine hiyo Ofisini kwake.

“Kwa kuwa mashine hii iliibiwa mchana na ikaibiwa na vifaa vyake vyote, inaonyesha kuwa waliohusika ni wataalamu na kwa maana hiyo watumishi wote 137 wa hospitali hii mnahusika na wizi huu, hivyo nyie ni watuhimiwa wa kwanza wa wizi huu. 


“Kila mmoja kuanzia kwa Mganga Mkuu wa Halmashuari mtachangia kulingana na kila mtu na mshahara wake, nataka ndani ya siku saba nikabidhiwe hiyo mashine, ambaye atagoma kuchangia huyo itakuwa halali yangu,” alisema Kiswaga.


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527