SADC YAANIKA SABABU TANZANIA KUPEWA NAFASI YA KUANDAA MKUTANO WA JUMUIYA YA MAENDELEO YA NCHI ZA KUSINI MWA AFRIKA 2019

Tanzania imepewa fursa ya kuwa mwenyekiti wa Jumuiya ya maendeleo ya nchi za kusini mwa Afrika (SADC) kutokana na kutimiza vigezo vinavyohitajika na jumuiya hiyo ikiwemo uwepo wa demokrasia na utawala bora mbali na vigezo vingine kama vile mchango wa Tanzania katika ukombozi wa bara la Afrika pamoja na uwepo wa uenyekiti wa awamu.

Hayo yamesemwa na Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo Dkt Stagomena Tax muda mfupi mara baada ya kumalizika kwa mkutano wa 21 wa kamati ya mawaziri kuhusu asasi ya siasa,ulinzi na usalama ya Jumuiya ya maendeleo kusini mwa bara la Afrika SADC kinachofanyika katika ukumbi wa mikutano wa kimataifa wa Mulungushi Lusaka nchini Zambia.

Amezitaka nchi wanachama wa jumuiya hiyo kuendelea kukuza demokrasia na utawala bora kwa kuwa ndio nguzo muhimu za jumuiya hiyo na kwamba licha ya uchanga wa demokrasia katika ukanda huo nchi hizo zimeendelea kupiga hatua kubwa katika kuboresha demokrasia na utawala bora na Tanzania ni mojawapo ya nchi zinazozingatia uwepo wa demokrasia na utawala bora miongoni mwa nchi wanachama. 

Mkutano huo wa mawaziri wa asasi ya siasa,ulinzi na usalama ya Jumuiya ya maendeleo kusini mwa Afrika SADC umeiridhishwa na ukuaji wa demokrasia na utawala bora miongoni mwa nchi wanachama kutokana na chaguzi zilizofanyika kwa haki,uhuru na Amani katika nchi takribani sita ikiwemo Afrika ya Kusini,Eswatini,Malawi,Madagascar pamoja na Jamhuri ya demokrasia ya Congo DRC.

Kwa upande wake Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Prof. Palamagamba John Kabudi amesema kumalizika kwa chaguzi katika nchi sita wanachama wa jumuiya hiyo kunaidhihirishia dunia namna ambavyo Ukanda wa Kusini mwa Afrika ukiyasimamia mambo yake yenyewe bila ya kuingiliwa na mataifa mengine,Afrika ina uwezo wa kuimarisha taasisi zake za demokrasia,utawala bora na haki jambo ambalo Tanzania inalisimamia kwa dhati na kwa umakini.

Ameongeza kuwa mkutano huo pia umejadili suala la maombi ya Burundi kuomba kujiunga na jumuiya ya maendeleo kusini mwa Afrika maombi ambayo yamekuwepo kwa takribani miaka mitatu sasa, na kutanabaisha kuwa Burundi imetekeleza kwa kiwango cha asilimia sabini masharti iliyotakiwa kuyatimiza ili kupata ridhaa ya kuwa mwanachama wa SADC na kwamba yale ya asilimia thelathini yaliyosalia,Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa kushirikiana na sekretarieti ya SADC na nchi nyingine wanachama zitaendelea kuisaidia Burundi ili iweze kuwa mwanachama jambo litakaloisaidia Burundi kuimarika kisiasa na kidemokrasia na kushiriki katika maendeleo ya Bara la Afrika.

Maazimio yote ya mkutano huo wa 21 wa kamati ya mawaziri kuhusu asasi ya siasa,ulinzi na usalama ya Jumuiya ya maendeleo kusini mwa bara la Afrika SADC sasa yatapelekwa katika mkutano wa wakuu wa nchi wanachama utakaofanyika Dar es Salaam nchini Tanzania mwezi Augusti mwaka huu ili wakuu hao wan chi waweze kufanya maamuzi ya mwisho kwa ajili ya utekelezaji.

Aidha Prof. Palamagamba John Kabudi ameitumia fursa ya mkutano huo kumweleza Katibu Mkuu wa SADC Dkt Stagomeana Tax kuhusu maandalizi ya mkutano wa SADC utakaofanyika Dar Es Salaam Tanzania ambaye ameonekana kuridhika na maandalizi hayo huku akiwasisitiza watanzania kuitumia fursa ya ujio wa wakuu wa Nchi 16 kwa pamoja Tanzania kwa ajili ya kujipatia kipato kupitia furtsa mbalimbali za kibiashara zitakazojitokeza katika mkutano huo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527