Picha : KANISA LA PAGT LATOA MSAADA KWA WATOTO WANAOISHI KATIKA MAZINGIRA MAGUMU KISHAPU

Kanisa la Pentecostal Assemblies of God Tanzania (P.A.G.T) limetoa msaada wa nguo na vifaa vya shule kwa wanafunzi wanaoishi katika mazingira magumu kata ya Mwadui Lohumbo wilayani Kishapu. 

Msaada huo umekabidhiwa wakati wa ibada maalumu ya kuwasaidia watoto wanaoishi katika mazingira magumu iliyofanyika Jumapili Januari 13,2019. 

Akikabidhi msaada huo Askofu wa kanisa la P.A.G.T Nyenze Mchungaji Robert Joseph aliiomba jamii pamoja na taasisi zisizo za kiserikali kuunga mkono juhudi za serikali kutoa misaada mbalimbali kwenye jamii, pia utoaji ni agizo la Mungu linaloashiria upendo kwa wahitaji. 

“Sababu Mungu anatupenda wote hivyo yatupasa kuwasaidia wahitaji na kwa kufanya hivyo tutakuwa tunaunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya tano ya kuwasaidia wanyonge,” alisema Joseph. 

Akizungumza kwenye ibada hiyo kwa niaba ya mkuu wa wilaya Kishapu Nyabaganga Talaba, Kaimu Afisa Maendeleo ya jamii wilaya ya Kishapu Ndola Masunga  aliwapongeza walezi ambao wamechukua jukumu la ulezi bila manyanyaso kwa watoto. 

“Tunashuhudia kwenye ofisi zetu za maendeleo ya jamii vihoja vingi vya kuwanyanyasa watoto wanaoishi mazingira magumu,niwapongeze walezi waliochukua jukumu la kuwalea watoto bila ya kuwanyanyasa na kuwapatia mahitaji muhimu,” alisema Ndola. 

Kanisa hilo limetoa msaada wa nguo na vifaa vya shule kwa wanafunzi wanaoishi mazingira magumu lengo ikiwa ni kuwasaidia wazazi na walezi.

Diwani wa kata ya Masengwa Nicodemas Simon alisema msaada huo ni chachu ya kufanya vizuri kimasomo kwa wanafunzi hao.

Na  Malaki Philipo- Malunde 1 blog
 Askofu wa Kanisa la P.A.G.T Nyenze Mchungaji Robert Joseph ameiomba jamii pamoja na taasisi zisizo za kiserikali kuunga mkono juhudi za serikali kutoa misaada mbalimbali kwenye jamii yenye wahitaji.. Picha zote na Steve Kanyefu-Malunde 1 blog
 Kaimu Afisa maendeleo ya jamii Wilaya ya Kishapu Ndola Masunga kwa niaba ya mkuu wa wilaya Kishapu Nyabaganga Talaba  akiwapongeza walezi ambao wamechukua jukumu la ulezi bila manyanyaso kwa watoto . 
Diwani wa Kata ya Masengwa Nicodemas Simon akisisitiza juu ya umuhimu wa  msaada huo huku akisema kuwa msaada  ni chachu ya kufanya vizuri kimasomo kwa wanafunzi hao.
      Baadhi ya watoto waliopatiwa msaada wakiwa kanisani.

Mgeni rasmi kaimu afisa maendeleo ya jamii wilaya ya Kishapu Ndola Masunga akikabidhi msaada kwa watoto hao kwa Mkuu wa Wilaya ya Kishapu Nyabaganga Talaba. 
Zoezi la kukabidhi msaada huo likiendelea.
 Baadhi ya Wazazi/walezi wa watoto hao wakifuatilia kwa umakini zoezi la utolewaji msaada kwa watoto hao


Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527