MKUU WA SHULE AMWADHIBU KWA KUMCHAPA MAKOFI MWALIMU MWENZAKE

Mkuu wa shule ya Sekondari Kabwe iliyopo Mwambao wa Ziwa Tanganyika wilayani Nkasi katika mkoa wa Rukwa , Jackson Mussa amemwadhibu mwalimu mwenzake Emanuel Mbemba kwa kumchapa makofi mbele ya wanafunzi.

Ofisa Elimu Kata ya Kabwe , Geofrey Mtafya amethibitisha kutokea kwa tukio hilo lililotokea jana Alhamis Februari 15,2018 asubuhi shule hapo na kusababisha taharuki kubwa kwa wanafunzi na jumuiya ya shule hiyo.

Akisimulia mkasa huo alisema kuwa asubuhi hiyo ya tukio Mwalimu Mbemba alikwenda kwenye ofisi ya Mkuu wa Shule Mussa na kumuomba ruhusa ili aende kwenye ziara ya mafunzo kwa kutembelea fukwe za Ziwa Tanganyika.

“Mwalimu Mkuu (Mussa ) alimtaka mwalimu huyo aandike barua ya kiofisi ambapo alifanya hivyo …… Mussa alimweleza mwalimu huyo kuwa baada ya muda si mrefu atampatia majibu kwa maandishi “ aliieleza Malunde1 blog .

Baadae Mwalimu Mbemba alimfuata mkuu wa Shule kufuatilia majibu yake lakini alielezwa kuwa aendelee kusubiri kwa kuwa alikuwa bado hajaiandika barua ya kumpatia ruhusa kutokana na kuwa na majukujmu mengine.

“Mwalimu Mbemba alimfuata mkuu wa Shule ikiwa ni mara ya tatu na alimweleza kuwa anachelewa kwenda kwenye ziara ya mafunzo na wanafunzi wa kidato cha tatu ….. ndipo mkuu wa shule alipotaharuki na kumkaba koo mwalimu huyo mbele ya wanafunzi na akaanza kumzaba vibao mfululizo “ alieleza .

Taarifa kutoka shuleni hapo zinaeleza kuwa wanafunzi na jumuiya ya shule hiyo walishuhudia tukio hilo huku baadhi yao wakishangilia na kuzomea.

Mtafya alisema kuwa Mwalimu Mbemba alitoa taarifa Kiongozi wa Chama Cha Walimu (CWT) mahali pa Kazi , Elia Elia ambaye alimtaarifu Ofisa Mtendaji Kata ya Kabwe Jofrey Kuzumbi ambaye aliitisha kikao cha dharura shuleni hapo .

Ofisa Elimu Sekondari wilaya ya Nkasi Abel Ntupwa alikiri kutokea kwa tukio hilo ambapo alilaani na kusisitiza kuwa ni utovu wa nidhamu huku akisema kuwa atalitolea maamuzi Jumatatu baada ya kupatiwa ripoti kamili.

Na Walter Mguluchuma -Malunde1 blog

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527