Kesi ya Uchochezi: Mbunge Lissu Amefikishwa Mahakamani,Wafuasi Wa Chadema Watiwa Mbaroni



June 29 2016 Mbunge wa Singida Mashariki ‘CHADEMA’ aliswekwa rumande katika kituo kikuu cha polisi, Dar es salaam kwa madai ya kutoa kauli ya uchochezi kwa kumuita Rais wa nchi ‘dikteta uchwara’.




Inadaiwa kwamba Tundu Lissu alitoa kauli hiyo ya uchochezi nje ya mahakama ya hakimu mkazi Kisutu wakati akizungumza na waandishi wa habari baada ya kesi yake nyingine inayomhusisha yeye na wenzake watatu wanaotuhumiwa kwa kauli za uchochezi kupitia gazeti la mawio kwa kuandika uchaguzi wa Zanzibar ungesababisha machafuko.



Leo June 30 2016 Tundu Lissu amesomewa shitaka lake la kutoa maneno ya uchochezi nje ya mahakama ya hakimu mkazi kisutu June 28 2016 kinyume cha kifungu namba 32 ya sheria ya magazeti. Lissu amekana shtaka hilo na ameachiwa kwa dhamana na hatotakiwa kusafiri nje ya nchi bila kibali cha mahakama.



Tundu Lissu anatetewa na mawakili 11 akiwemo John Mallya na Peter kibatara wakati upande wa Jamhuri una mawakili watatu wanaosimamia kesi hiyo, kesi hiyo itasikilizwa August 02 2016.

Tundu Lissu, Mbunge wa Singida Mashariki amesema, ‘namtaka dikteta uchwara mahakamani,’.


Lissu ambaye ni Mnadhimu wa Kambi Rasmi ya Upinzani Bungeni amesema hayo leo muda mfupi baada ya kutoka kusikiliza shauri lake katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu, jijini Dar es Salaam la kudaiwa kutoa kauli ya uchochezi.


“Mimi na jopo langu la mawakili tunamtaka niliyemuita diktekta uchwara aje mahakamani kuthibitisha udikitekta uchwara wake,” amesema Lissu.


Lissu amefunguliwa shitaka la uchochezi katika mahakama hiyo, kesi yake inasikilizwa na Hakimu Yohona Yongolo ambapo kwa upande wa mashitaka, unawakilishwa na Benard Kongolo, wakili wa serikali mkuu.


Lissu alijisalimisha jana 5 asubuhi katika kituo hicho cha polisi ambapo alizuiliwa kupewa dhama na kulala hadi alipofikishwa mahakamani leo.


Wafuasi na viongozi mbalimbali wa Chadema walifika mahakamani hapo akiwemo Freeman Mbowe, Mwenyekiti wa chama hicho taifa; Salum Mwalim, Kaimu Katibu Mkuu Zanzibar na Benson Kigaila, Mkuu wa Operesheni wa chama hicho.


Wakili Kongolo amedai kuwa, Lissu alitenda kosa hilo tarehe 28 Juni mwaka huu katika eneo la Mahakama ya Kisutu jijini Dar es Salaam kwa kuzungumza;


“Mamlaka ya Serikali mbovu ni ya kidiktekta uchwara inahitaji kupingwa na kila Mtanzania kwa nguvu zote, huyu dikitekta uchwara lazima apingwe kila sehemu kama uongozi utafanywa na utawala wa kijinga nchi inaingia ndani ya giza nene.’’


Hata hivyo, Lissu amekana shitaka hilo, amedhaminiwa na wadhamini wawili waliosaini hati ya Sh.2 milioni kila mmoja na masharti ya kutosafiri nje ya nchi na kwamba, upelelezi wa kesi hiyo umekamilika. Kesi hiyo itatajwa kwa kusikilizwa tarehe 2 Agosti mwaka huu.


Upande wa utetezi uliwakilishwa na mawakli 11 miongoni mwao ni Michael Ngolo, Peter Kibatala, John Mallya, Hekima Mwasibu, Omari Msemo, Jeremia Mutasebya na Juma Nasoro.


Nje ya Mahakama
Alipotoka nje ya mahakama Lissu alizungumza na wafuasi wa Chadema waliofurika katika viwanja hivyo pamoja na waandishi wa habari ambapo amesema, “nilijua kwamba wenye busara watanyamaza baada ya mimi kutoa kauli ile juzi mahakamani hapa."


Hata hivyo, Lissu amesema kuwa, katika kituo alicholazwa ameshuhudia watu wakiteseka kutokana na kutopelekwa mahakamani kwa muda wa wiki mbili hadi mwezi mmoja na kuwa, hupewa mateso makali mpaka kusababisha wengine kuvunjwa miguu.


Mbowe amewaambia waandishi wa habari kuwa, uonevu wa utawala wa sasa unafanywa bungeni na nje ya bunge na kwamba, hawatakata tamaa ya kupigania haki.


Wakati huo huo Jeshi la Polisi limewatia mbaroni wafuasi wanne wa Chadema walikuwa wamebeba mabango yenye maneno ‘Dikitekta Uchwara nenda Burundi,’ Polisi ‘Uchwara acheni kutumika’ na ‘Lisuu Tanzania inakuhitaji.’
Chanzo-Mpekuzihuru na Millardayo.com

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527