MAKAMU Mwenyekiti wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Tanzania Baraa, Stephen Wasira, ameiagiza Mamlaka ya Majisafi na Usafi wa Mazingira Same (SAUWASA) kuhakikisha inatatua kwa haraka changamoto ya upatikanaji maji inayowakabili wananchi wa mji wa Same.
Wasira alitoa agizo hilo leo Juni 8, 2026 alipokuwa akizungumza na wanachama wa CCM wa Shina Namba 9, Tawi la Same, Kata ya Same, wilayani Same mkoani Kilimanjaro.
Akijibu malalamiko ya wananchi kuhusu ukosefu wa maji, alisema haikubaliki kwa wakazi wa Same kuendelea kukosa huduma hiyo muhimu wakati maji yanapatikana kwa wingi kupitia miradi iliyotekelezwa na serikali.
“Ninaiagiza SAUWASA kuhakikisha wananchi wa Same wanapata maji. Haiwezekani watu wa Same waendelee kuyasikia au kuyaona maji bila kuyapata kwa matumizi yao ya kila siku, mfumo wa usambazaji uharakishwe ili wananchi wanufaike na huduma hiyo muhimu,” alisema Wasira.
Alibainisha kuwa, serikali imewekeza fedha nyingi kutekeleza mradi wa maji wa Same–Mwanga–Korogwe, hivyo hakuna sababu ya wananchi kuendelea kukosa huduma hiyo kutokana na changamoto za usambazaji.


Social Plugin