Meneja wa CRDB Bank Kanda ya Magharibi Jumanne Wagana akikabidhi msaada wa madawati 40 shule ya msingi Tindenghulu Halmashauri ya Shinyanga
Stella Herman,Shinyanga
CRDB Bank imeendelea kuunga mkono jitihada za kuboresha mazingira ya elimu kwa kutoa msaada wa madawati 40 kwa Shule ya msingi Tindenghulu iliyopo Kata ya Usule, Wilaya ya Shinyanga, ikiwa ni sehemu ya utekelezaji wa kampeni yake ya “Keti Jifunze” inayolenga kuboresha mazingira ya kujifunzia kwa wanafunzi.
Akizungumza wakati wa hafla ya
kukabidhi madawati hayo Juni 1, 2026, Meneja wa CRDB Bank Kanda ya Magharibi, Jumanne Wagana, amesema msaada huo ni
sehemu ya utaratibu wa Banki hiyo wa kurejesha sehemu ya faida yake kwa jamii
kupitia shughuli mbalimbali za maendeleo.
Amesema madawati hayo yatachangia
kuondoa changamoto ya wanafunzi kusoma wakiwa wamekaa chini, jambo
litakaloongeza ari ya kujifunza, kuboresha usikivu darasani na kuwawezesha
walimu kufundisha katika mazingira bora zaidi.
“Tunashiriki katika kusaidia sekta
mbalimbali ikiwemo elimu, afya, mazingira na maeneo mengine ya kijamii,
Tunatambua kuwa Serikali ina majukumu mengi ya kuhudumia wananchi, hivyo sisi
kama wadau wa maendeleo tunaona ni muhimu kutoa mchango wetu katika kupunguza
changamoto zilizopo,” amesema Wagana
Aidha, amewaomba wananchi kuendelea
kutumia huduma za CRDB Bank ili kuongeza uwezo wa Banki hiyo kuendelea
kurejesha sehemu ya mapato yake kwa jamii kupitia miradi ya maendeleo.
“Ninawaomba muendelee kutumia huduma
za CRDB Bank Kadri matumizi ya huduma zetu yanavyoongezeka, ndivyo tunavyopata
uwezo mkubwa zaidi wa kuendelea kusaidia jamii kupitia miradi mbalimbali ya
maendeleo,”amesema Wagana
Wagana amesema kuwa CRDB Bank inaendelea kutoa huduma mbalimbali za kifedha zikiwemo mikopo yenye masharti nafuu kwa wakulima, wafugaji na wafanyabiashara, huku akisisitiza kuwa benki hiyo ipo kwa ajili ya Watanzania wote na ina jukumu la kusaidia ukuaji wa uchumi wa wananchi.
Kwa upande wake, mwakilishi wa Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga ambaye pia ni Katibu Tawala wa Wilaya hiyo, Said Kitinga, ameipongeza CRDB Bank kwa kuendelea kuwa mstari wa mbele kusaidia jamii kupitia miradi ya maendeleo katika sekta mbalimbali.
Amesema msaada huo ni mfano wa ushirikiano mzuri kati ya sekta binafsi na Serikali katika kuboresha huduma za kijamii, hususan elimu.
Kitinga amewataka wanafunzi kuyatunza madawati hayo kwa kuepuka kuyaharibu kupitia matumizi yasiyo sahihi, ikiwemo kuruka juu yake, huku akisisitiza umuhimu wa kuyafanyia matengenezo madawati yanayoharibika ili yaweze kudumu kwa muda mrefu.
Naye Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya ya Shinyanga, Sethi Msangwa, amesema tatizo la upungufu wa madawati bado ni changamoto katika baadhi ya shule za halmashauri hiyo, hivyo msaada wa CRDB Bank umekuja kwa wakati muafaka na umechangia kupunguza tatizo hilo.
Amebainisha kuwa ushirikiano wa wadau wa maendeleo kama CRDB Bank ni muhimu katika kusaidia juhudi za Serikali za kuboresha sekta ya elimu na kuhakikisha wanafunzi wanapata mazingira bora ya kujifunzia.
Social Plugin