Na Stella Herman,SI Media
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Julius Mtatiro ameanza kuchukuwa hatua kwa taasisi za fedha zinazokopesha fedha kisha kwenda kubeba vitu vya watu mtaani wanapokuwa wamechelewa kurejesha mikopo jambo ambalo ni kinyume cha sheria na taratibu.
Hatua hiyo imechukuliwa kufuatia kuenea kwa mikopo umiza maarufu kama kausha damu, inayotolewa na baadhi ya taasisi na watu binafsi kwa riba kubwa, huku wakopaji wakikumbwa na vitisho na mali zao kuchukuliwa wanaposhindwa kurejesha kwa wakati.
Mkuu wa Wilaya ya Shinyanga Julius Mtatiro ametoa agizo wakati wa kikao na wadau mbalimbali zikiwemo taasisi za fedha,amesema vitendo vya kunyanyasa wananchi havikubaliki na nilazima kuchukuwa hatua.
Amesisitiza kuwa ni marufuku kwa mkopeshaji yeyote kuchukua mali za mkopaji bila kufuata taratibu za kisheria, akibainisha kuwa njia sahihi ni kufungua shauri mahakamani ili kupata uamuzi halali.
Mwanasheria wa Halmashauri ya Manispaa ya Shinyanga, Rose Matunda, amesema wapo watu wanaojihusisha na utoaji mikopo bila kuwa na vibali halali, jambo linalochangia ukiukwaji wa sheria na unyonyaji kwa wananchi.
Amesema mikataba ya mikopo inapaswa kuwa wazi na rahisi kueleweka kwa pande zote, lakini mara nyingi wakopaji hawapewi nafasi ya kuelewa masharti kabla ya kusaini.
Alisisitiza umuhimu wa kuweka usimamizi madhubuti ili kuhakikisha mikopo inatolewa kwa kuzingatia sheria na haki za wananchi zinalindwa.
Social Plugin