
Kupitia taarifa kwa umma iliyotolewa Machi 5, 2026, wananchi hao wamesema bado wanasubiri kwa hamu majibu kutoka kwenye tume hizo ambazo ziliundwa Februari 2025 kwa lengo la kuchunguza kwa kina migogoro ya ardhi inayojitokeza katika eneo la Ngorongoro.
Pamoja na hilo, tume hizo pia zilipewa jukumu la kutathmini mpango wa kuhamisha baadhi ya wakazi kutoka eneo la Hifadhi ya Ngorongoro kwenda kijiji cha Msomera kilichopo mkoani Tanga, hatua ambayo imekuwa ikizua mjadala mkubwa miongoni mwa wananchi.
Pia Kwa mujibu wa taarifa hiyo, tume hizo zilipewa muda wa siku tisini kukamilisha kazi yake na kuwasilisha ripoti kwa Serikali, ambapo muda huo ulitarajiwa kumalizika Mei 2025. Hata hivyo, hadi sasa ripoti hizo bado hazijawekwa wazi jambo ambalo limezua sintofahamu kwa wakazi wa eneo hilo.
Aidha Wananchi wamesema kuchelewa kwa ripoti hizo kunazidi kuongeza hofu na mashaka, huku wengi wakitarajia majibu yatakayosaidia kupatikana kwa suluhisho la kudumu la migogoro ya ardhi ambayo imekuwa ikiathiri maisha yao kwa muda mrefu.
Wameitaka Serikali kuhakikisha kuwa maamuzi yatakayofanyika yanazingatia maoni ya wananchi wa Ngorongoro, pamoja na kulinda haki zao za msingi na ustawi wa maisha yao.
Hata hivyo, wananchi hao wameeleza kuwa wanatarajia majibu ya wazi na yenye kuleta matumaini, ili hatimaye kupatikana kwa njia sahihi ya kumaliza changamoto za ardhi zinazolikabili eneo hilo.



Social Plugin