Habari Mpya

6/recent/ticker-posts

MAHAFALI YA 19 YA KIDATO CHA NNE SHULE YA SEKONDARI RWEPAS

Wanafunzi wa shule ya sekondari Rwepas, wilayani Kahama mkoani Shinyanga, wameshauriwa kuendelea kupenda na kusoma masomo ya sayansi kutokana na nafasi yake kubwa katika kujiajiri na kuajiriwa mara baada ya kuhitimu masomo yao.

Ushauri huo umetolewa na mgeni rasmi, Ofisa Mkaguzi na Mdhibiti Ubora wa Shule Manispaa ya Kahama, Lazaro Malili, katika mahafali ya 19 ya kidato cha nne yaliyofanyika shuleni hapo. Malili amesema bado kuna changamoto ya baadhi ya wanafunzi kuogopa kusoma masomo ya sayansi licha ya fursa nyingi zilizomo ndani yake.

Akizungumza katika hafla hiyo, Malili amesema serikali imeweka mitaala miwili ya elimu mkondo wa amali na mkondo wa ujumla ambayo humwezesha mwanafunzi kusoma kile anachokipenda, huku akibainisha kuwa masomo ya sayansi yana mchango mkubwa katika maisha ya kila siku. “Masomo ya sayansi yamebeba fani nyingi ikiwemo uhandisi, udaktari, kilimo cha mifugo, kilimo cha mazao na utunzaji wa mazingira. Mwanafunzi akiyapenda na kuyamudu vizuri, anaweza kujiajiri bila kusubiri kuajiriwa,” amesema Malili.

Kwa upande wake, Mhandisi Happines Malila kutoka Chuo cha Madini Shinyanga, amewatia moyo wanafunzi wa kike kusoma masomo ya sayansi bila woga, akisema dhana kwamba ni masomo ya wavulana pekee si sahihi. “Nilipambana, nikavumilia changamoto na sasa naona matunda ya juhudi zangu. Hivyo basi, nawaomba msisite kuyapenda masomo haya,” amesema.

Aidha, wazazi waliokuwa sehemu ya mahafali hayo, akiwemo Monica Julius na Biles Ntangalo, wamewashauri wanafunzi wahitimu kuepuka makundi mabaya mitaani na badala yake wajitunze wakisubiri matokeo ya mitihani yao. 

Nao baadhi ya wahitimu, Agnes Patrick na Alphan Majid, walisema wamechagua masomo ya sayansi kwa hiari kwa kuwa yanaendana na vipaji vyao na yatawasaidia hata katika maisha ya nyumbani.

Mkurugenzi wa shule hiyo, Frank Samweli, amesema kwa sasa shule ina jumla ya wanafunzi zaidi ya 500 kuanzia kidato cha kwanza hadi cha nne, ambapo wahitimu wa mwaka huu ni 73 wasichana 40 na wavulana 33 na matarajio ni wote kufaulu na kujiunga na kidato cha tano pamoja na vyuo.

 






















































MMMM

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundeblog@gmail.com