NECTA YAFUTA MATOKEO YA WALIOANDIKA MATUSI, KUINGIA NA VIBOMU, SIMU KWENYE MTIHANI

 

MATOKEO YA MTIHANI WA KIDATO CHA NNE(CSEE) 2023 NA MTIHANI WA MAARIFA (QT) YAMETANGAZWA RASMI LEO ALHAMISI JANUARI 25,2024

MATOKEO YA MTIHANI WA KIDATO CHA NNE (CSEE) 2023

MATOKEO YA MTIHANI WA MAARIFA (QT) 2023


Wanafunzi watano wamefutiwa matokeo ya Mtihani wa Kidato cha Nne 2023 baada ya kuandika matusi kwenye karatasi zao za mtihani huku watahiniwa 102 wakifutiwa matokeo baada ya kubainika kuwa walifanya udanyanyifu kwenye mtihani.


"Hili ni suala la maadili, pamoja na hatua tutakazochukua kwa kuandikia shule nzima tutataka wakuu wa shule wawafuatilie hawa wanafunzi, tunasisitiza kwenye kuelimisha wanafunzi wa madarasa ya chini waone hatari ya jambo hilo",  amesema Katibu Mtendaji wa Baraza la Mitihani Tanzania (Necta), Dkt. Said Mohamed wakati akitangaza matokeo ya mtihani huo leo, Alhamisi Januari 25, 2024. 

“NECTA imefuta matokeo ya watahiniwa watano wa kidato cha nne walioandika lugha ya matusi katika skripti zao. Matokeo hayo yamefutwa kwa mujibu wa Kifungu cha 5 (2) (j) cha sheria ya Baraza la Mitihani sura ya 107 kikisomwa pamoja na Kifungu cha 30(2) (b) cha Kanuni za Mitihani Mwaka 2016",amesema.

Amesema pia NECTA imewafutia matokeo watahiniwa 102 baada ya kubainika kuwa walifanya udanyanyifu kwenye mtihani.

"Hawa tuliowafutia matokeo tulibaini ni wao wenyewe ndiyo walifanya udanganyifu, wapo walioingia na simu kwenye chumba cha mtihani, wapo waliokutwa na notisi (Vibomu) na wengine walikuwa wakisaidiana. Lakini pia tumemkamata mwalimu mkuu ambaye alikuwa akiwasaidia wanafunzi wake, huyu hatua zimeshachukuliwa. Kwa kifupi mwaka huu hatujafungia kituo chochote cha mtihani kwa kuwa udanganyifu umefanywa na watu binafsi", amesema Dkt. Mohamed.

NECTA pia limezuia kutoa matokeo ya watahiniwa 376 ambao walipata matatizo ya kiafya na kushindwa kufanya mitahani yote au idadi kubwa ya masomo hivyo wamepewa nafasi ya kuyafanya kwa mwaka wa masomo 2024.


 "Watahiniwa husika wamepewa fursa ya kufanya mtihani kwa masomo ambayo hawakuyafanya kwa sababu ya ugonjwa mwaka 2024 kwa mujibu wa Kifungu cha 32(1) cha Kanuni za Mitihani”, amesema Dkt.Mohamed. 

Amesema, katika mtihani huo jumla ya watahiniwa 484,823 sawa na asilimia 87.65 ya watahiniwa waliofanya mtihani wamefaulu. 

“Wasichana waliofaulu ni 257,892 sawa na asilimia 86.17 wakati wavulana waliofaulu ni 226,931 sawa na asilimia 89.40, mwaka 2022. Watahiniwa waliofaulu walikuwa ni 476,450 sawa na asilimia 86.78, hivyo ufaulu wa watahiniwa umeongezeka kwa asilimia 0.87 ikilinganishwa na mwaka 2022.

 Kati ya wanafunzi hao waliofaulu kuna watahiniwa wa shule na watahiniwa wa kujitegemea ambapo jumla ya watahiniwa wa shule 471,427 kati ya 527,576 wenye matokeo ambao ni sawa na asilimia 89.36 wamefaulu ambapo wamepata madaraja ya I, II, III na IV.  Mwaka 2022 watahiniwa waliofaulu walikuwa 456,975 sawa na asilimia 87.79, hivyo ufaulu umeongezeka kwa asilimia 1.57. 

“Watahiniwa wa kujitegemea waliofaulu mtihani ni 13,396 sawa na asilimia 52.44, mwaka 2022 watahiniwa wa kujitegemea 19,475 sawa na asilimia 68.34 walifaulu mtihani huo, hivyo ufaulu wa watahiniwa hao wa kujitegemea umeshuka kwa asilimia 15.90 ukilinganisha na mwaka 2022”, amesema Katibu Mtendaji huyo.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553
Previous Post Next Post