RAIS SAMIA APEWA HESHIMA SEATTLES KWA KUTANGAZA UTALII



Lumen Field, Seattle

Mashabiki takribani 31,620 waliohudhuria mechi ya Ligi Kuu ya Soka ya Marekani na mamilioni zaidi duniani waliokuwa wakitazama “live” mechi ya Seattle Sounders dhidi ya Sporting Kansas City kupitia FOX TV na Apple TV, wamepata fursa ya kushuhudia Rais Samia Suluhu Hassan wa Tanzania akienziwa katika tukio maalum kabla ya mechi hiyo kuanza mjini humo jana Jumapili Mei 7, 2023. 

Mmiliki wa Seattle Sounders, Bilionea Adrian Hanauer, aliamua kutumia mechi hiyo kufanya tukio la kumpongeza Rais Samia kwa hatua zake za kutangaza utalii wa Tanzania hasa kupitia filamu ya Royal Tour.


Kwa heshima hiyo, Hanauer jana alitumia mechi hiyo kukabidhi jezi maalum yenye jina la Rais Samia kwa Katibu Mkuu Wizara ya Utalii, Dkt. Hassan Abbasi na ujumbe wake na zaidi kutoa heshima kwa ujumbe wa Tanzania kupiga picha maalum na kikosi cha Sounders kabla ya kuanza kwa mechi hiyo muhimu. 


“Lengo la tukio hili maalum kwa Rais wa Tanzania ni kutambua mchango wake katika kutangaza utalii. Niliwahi kutoa mchango mwingine kwa kuileta timu hii mwaka 2005 Tanzania ikacheza na klabu kubwa za Simba na Yanga na tutaangalia tena jinsi ya kufanya ziara nyingine ya kiutalii kuja Tanzania na wachezaji wetu,” alisema Bw. Hanauer.


“Tukio hili ni heshima kubwa kwa Rais Samia, nchi yetu Tanzania na utalii wa Tanzania kwani mamilioni ya watu waliofuatilia leo matukio ya uwanjani watazidi kujihusisha na Brand ya Tanzania na kuja nchini,” alisema Dkt. Abbasi akiwa uwanjani hapo. 


Tukio la jana linakuja ikiwa ni siku chache tu baada ya juzi ambapo wamiliki wa Seattle Sounders walitoa fursa nyingine ya kuutangaza utalii wa Tanzania katika sehemu ya uwanja huo kwa kuionesha filamu ya “Tanzania; The Royal Tour” kwa wawakilishi wa makampuni makubwa duniani kama Google, Boeing, Starbucks, Amazon, Delta na Microsoft na ofisi ya Meya wa Seattle.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments