SERIKALI YAONYA UBADILISHAJI MATUMIZI YA ARDHI BILA SABABU ZA MSINGI

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula akizungumza katika Kikao kazi kilichowaunganisha wakurugenzi wa Halmashauri na watalaam wa Sekta ya Ardhi nchini kilichofanyika jijini Dodoma Oktoba 1, 2022. Sehemu ya washiriki wa kikao kazi kilichowaunganisha wakurugenzi wa Halmashauri na watalaam wa Sekta ya Ardhi nchini kilichofanyika jijini Dodoma Oktoba 1, 2022. Katibu Mkuu Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Allan Kijazi akizungumza katika kikao kazi kilichowaunganisha wakurugenzi wa Halmashauri na watalaam wa Sekta ya Ardhi nchini kilichofanyika jijini Dodoma Oktoba 1, 2022.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Dkt Angeline Mabula (wa tatu waliokaa mbele ) na viongozi wengine wakiwa katika picha ya pamoja na baadhi ya wakurugenzi wa halmashauri walioshiriki Kikao kazi kati ya wakurugenzi wa Halmashauri na watalaam wa Sekta ya Ardhi nchini kilichofanyika jijini Dodoma Oktoba 1, 2022.

****************************

Na Munir Shemweta, WANMM DODOMA

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe Dkt Angeline Mabula amezionya halmashauri nchini kuacha utaratibu wa kubadilisha matumizi ya ardhi bila sababu za msingi.

Dkt Mabula alitoa onyo hilo Oktoba 1, 2022 jijini Dodoma wakati wa kuhitimisha kikao kazi kilichowaunganisha wakurugenzi wa Halmashauri na wataalamu wa sekta ya ardhi kilichofanyika jijini Dodoma.

" Sasa hivi kila mmoja anaondoa open space anataka kupima viwanja anafuta mashamba anataka kupima viwanja hata kama bado yako katika sura ya kijijini ya kimashamba na anataka kila sehemu kuwe fremu"

Akitolea mfano wa jiji la Dodoma, Dkt Mabula alisema, jiji hilo limeanza kusheni fremu wakati ni Makao makuu ya nchi na kusema haiwezekani kuwa na miji ya aina hiyo ambayo haipangwi kwenye sura ya makao makuu kwa kujaza fremu na vituo vya mafuta na kusisitiza kuwa hiyo si sahihi kitaaluma.

Kwa mujibu wa Waziri wa Ardhi, wapo wataalamu wengi katika sekta ya mipango miji na mabadiliko ya matumizi yasiyo na sababu za msingi hayakubaliki kwa kuwa yanawakosesa hata watoto maeneo ya kucheza sambamba na miji kupumua.

"Mipango iliyopangwa awali inatakiwa kubaki siyo kuendekeza mabadiliko ya matumizi kwa kujaza fremu au vituo vya mafuta na kuharibu miji, tunahitaji pia maeneo ya matumizi ya umma". Alisema Dkt Mabula

Kupitia kikao hicho kilichohudhuriwa pia na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais TAMISEMI Prof Riziki Shemdoe na Katibu Mkuu Ofisi ya Rais Menejimenti ya Tumushi wa Umma na Utawala Bora Laurean Ndumbaro, Dkt Mabula aliwataka Wakurugenzi ambao halmashauri zao tayari zina mipango kabambe kutoruhusu ujenzi kuendelea kwenye maeneo yao bila kuzingatia mipango hiyo na kusisitiza umuhimu wa maeneo kutunzwa kwa kuzingatia mipango kabambe badala ya kufuata mkumbo wa kutaka kubadili matumizi ya ardhi na kuharibu sura ya miji.

Kikao Kazi kati ya wakurugenzi wa halmashauri na wataalamu wa sekta ya ardhi kimefanyika kwa lengo la kupata maoni juu ya muundo mpya wa utendaji kazi wa wataalam wa ardhi katika ngazi ya Halmashauri.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments