KIKWETE AKUTANA NA WAGOMBEA URAIS KENYA ODINGA NA RUTO...UCHAGUZI MKUU KESHO!

Mheshimiwa Rais Mstaafu Dkt. Jakaya Kikwete akiwa Kiongozi ya Timu ya Uangalizi ya Uchaguzi wa Kenya, ya Jumuiya ya Afrika Mashariki, kwa nyakati tofauti, amekutana na kufanya mazungumzo na Wagombea Urais William Ruto kutokea Umoja wa Vyama vya Kenya Kwanza, na Raila Odinga wa Umoja wa Vyama vya Azimio la Umoja. Mgombea wa wa Azimio la Umoja Raila Odinga, aliambatana pia na Mgombea wake Mwenza Martha Karua.

Wagombea hao Naibu Rais William Ruto na Raila Odinga, kiongozi mkongwe wa upinzani ambaye sasa anaungwa mkono na chama tawala, wanapigania nafasi ya kuliongoza taifa hilo la Afrika Mashariki.

Wapiga kura wapatao milioni 22.1 kesho siku ya Jumanne tarehe 9,2022 watamchagua rais ajaye, atakayechukua nafasi ya rais Uhuru Kenyatta anayemaliza muda wake baada ya kuliongoza taifa la Kenya kwa mihula miwili. Kwa mujibu wa katiba Uhuru Kenyatta haruhusiwi kugombea muhula wa tatu baada ya kumaliza mihula miwili. 

Vilevile wakenya watawachagua maseneta, magavana, wabunge, wawakilishi wa wanawake na idadi ya maafisa 1,500 wa kaunti.


Matokeo rasmi yatatangazwa ndani ya wiki moja baada ya zoezi la kupiga kura. Ili kushinda moja kwa moja, mgombea anahitaji kupata zaidi ya nusu ya kura zote na angalau asilimia 25 ya kura katika zaidi ya nusu ya kaunti 47 za nchini Kenya. Iwapo hakutakuwepo na mshindi wa moja kwa moja maana yake ni uchaguzi wa marudio utakafanyika ndani ya siku 30.




Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments