CWT BAGAMOYO WALIA NA KIKOKOTOO

Viongozi mbalimbali wa Wilaya wakiwa kwenye tuzo ya Elimu ya halmashauri ya Bagamoyo
Katibu wa CWT Wilaya ya Bagamoyo Mwl. Shaaban Tessua akitoa salamu za chama

Na Elisante Kindulu - Bagamoyo

CHAMA Cha Walimu Tanzania(CWT) wilaya ya Bagamoyo kimeiomba serikali kuangalia upya uamuzi wake kwa kikokotoo kipya ambacho hakina tija kwa watumishi wa umma hususani walimu.


Hayo yalibainishwa na Katibu wa Chama Cha walimu Wilaya ya Bagamoyo , Mwl. Shaaban Tessua alipokuwa akitoa taarifa fupi kwenye siku ya tuzo za Elimu kwa halmashauri ya Bagamoyo lililofanyika katika viwanja vya Mwanakalenge mjini hapa  jana


Mwl. Tessua amesema kila ziara ambayo amekuwa akiifanya mashuleni kwa kuambatana na wajumbe wa kamati za utendaji na uendeshaji za Wilaya , moja kati ya kilio kikubwa kwa walimu ni kikokotoo kipya.


Mwl. Tessua alizitaja kero zingine ambazo walimu wamekuwa wakizipigia kelele kuwa ni  pamoja na baadhi yao kuchelewa kulipwa Fedha za mapunjo ya mshahara mara baada ya kupanda madaraja(arreas).

"Tumekuwa tukifanya ziara za mara kwa mara katika shule za msingi na Sekondari. Walimu wanalalamika mno juu ya kikokotoo, kuchelewa kulipwa arreas , ucheleweshwaji wa Fedha za nauli za likizo , Fedha za masomo, matibabu, mazishi na wakati mwingine hata uhamisho", alisema Katibu huyo.

Aidha Katibu huyo amezitaja mamlaka husika kupitia mikataba ya walimu wa shule binafsi na za serikali yenye changamoto kwa lengo la kuirekebisha.

Kwa upande mwingine Katibu huyo amewashauri walimu kufanya kazi kwa kuzingatia sheria, kanuni, miongozo, na maelekezo ili kukwepa kuingia katika  hatia.


Siku ya tuzo katika halmashauri ya Bagamoyo imeratibiwa na idara za Elimu msingi pamoja na Sekondari kwa lengo la kuwapongeza walimu kwa kuongeza kiwango Cha ufaulu katika mitihani ya Taifa kwa mwaka 2021.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments