MISA TAN YAWAJENGEA UWEZO WANAHABARI WA LINDI KUZIFAHAMU SHERIA ZA HABARI


Jesse Kwayu

Taasisi ya Vyombo vya Habari Kusini mwa Afrika tawi la Tanzania (MISA TAN) kwa kushirikiana na shirika la Kimataifa la Kuwezesha Vyombo vya Habari (IMS) imeendesha semina ya siku moja ya kuwajengea uwezo waandishi wa habari mkoani Lindi ili kuzielewa sheria za vyombo vya habari utakaowawezesha kushiriki kikamilifu katika mchakato wa marekebisho ya Sheria hizo.


Katika semina hiyo wanahabari wamepitia na kujadili vipengele mbalimbali vya Sheria vinavyokandamiza uhuru wa vyombo vya habari na kujieleza pamoja na haki ya kupata taarifa.


Mwezeshaji wa mafunzo hayo, Jesse Kwayu amewahimiza washiriki kujitokeza kutoa mapendekezo yatakayoboresha vifungu korofi vya sheria na kupata sheria nzuri kwa ustawi wa tasnia ya habari nchini.


"Kwa kuzifahamu sheria mtaweza kuwa mstari wa mbele kujadiliana changamoto mbalimbali za sheria hizi kwani hakuna mtu atakuja kutoka nje kuzungumzia changamoto unazokumbana nazo. Wewe ndiye unayeumizwa na hizi sheria na ndiye mwenye jukumu la kutafuta njia ya kuzitatua",Bw. Kwayu amesisitiza.

Kwa upande wao waandishi wa habari walioshiriki semina hiyo wameishukuru MISA TAN kwa kuwaongezea ujuzi wa kuzifahamu vyema sheria za habari nchini utakaowawezesha kutekeleza majukumu yao ya kihabari kwa weledi mkubwa. "Kupitia semina hii tumenufaika sana kujua vifungu kandamizi vya sheria mbalimbali ikiwemo EPOCA na Sheria ya Huduma ya Habari. Uwezo tuliojengewa utatuwezesha kushiriki kikamilifu katika zoezi la maboresho ya sheria hizi", amesema mwakilishi wa washiriki hao.


Semina hii iliyofanyika Lindi mjini imewanufaisha zaidi ya waandishi 30 wa mkoani humo nimuendelezo wa jitihada za MISA TAN kwa kushirikiana na IMS ya kuwafunda wanahabari kuzifahamu sheria zinazoongoza tasnia ya habari nchini Tanzania.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments