TAASISI YA TEKNOLOJIA YA DAR ES SALAAM (DIT) YATOA MSAADA WA VIATU KWA WANAFUNZI WANAOISHI KATIKA MAZINGIRA MAGUMU ILEMELA


Taasisi ya Teknolojia ya Dar es salaam (DIT) Kampasi ya Mwanza imekabidhi Jozi 126 za viatu vya ngozi kwa wanafunzi 126 wanaoishi kwenye mazingira magumu Manispaa ya Ilemela mkoani Mwanza.

Mkurugenzi wa Taasisi hiyo Dkt. Albert Mmari amesema Viatu hivyo vyenye thamani ya zaidi ya shilingi millioni tatu vimetengenezwa na wanafunzi pamoja na wajasiriamali wanaopata elimu kwenye Taasisi hiyo na vimetolewa ili kuwezesha wanafunzi hao kupata elimu bila kikwazo chochote.

“Serikali ya Rais Samia Suluhu Hassan imewekeza fedha nyingi kwenye sekta ya elimu ikiwemo kujenga madarasa zaidi ya elfu 15 kupitia fedha za UVIKO -19, DIT tumeamua kuunga mkono juhudi hizo kwa kutoa viatu ili kuwezesha kila mtoto kupata elimu kwenye mazingira bora”,alisema Dkt. Mmari wakati wa kukabidhi viatu kwa wanafunzi.

Aidha Dkt. Mmari amesema kuwa mkakati wa Taasisi ya Teknolojia ya Dar es salam kampasi ya mwanza ni kuwafikia wanafunzi wengi zaidi wanaotoka kwenye familia zisizojiweza.

“Hii ni awamu ya pili ya ugawaji wa viatu kwa wanafunzi wanaoishi kwenye mazingira magumu na hatutaishia hapa bali tutaendelea kugawa viatu ambapo baada ya kumaliza wilaya ya ilemela,tutaendelea na zoezi hilo katika wilaya zote za mkoa wa mwanza”,aliongeza Dkt. Mmari.

Wanafunzi 126 walionufaika na msaada huo wa viatu wanatoka kwenye shule za msingi Sangabuye,Nyafula na Bugogwaambao wameishukuru DIT kwa kuwawezesha kuondokana na changamoto ya ukosefu wa viatu iliyokuwa inawakabili.

“Naishi na bibi yangu ambaye hana uwezo wa kuninunulia kiatu lakini kwa msaada huu nitakuwa nahudhuria shuleni kila mara make zamani nilikuwa mtoro kwa sababu sikuwa na kiatu”,alisema mmoja kati ya wanafunzi 26 walionufaika na viatu hivyo katika shule ya msingi Bugogwa.

Kwa upande wao,uongozi wa shule za msingi Sangabuye,Bugogwa na Nyafula mbali na kuishukuru kwa dhati DIT wamesema msaada huo utasaidia kwa kiasi kukubwa kupunguza tatizo la utoro wa wanafunzi.

“Tuna watoto wengi wenye mahitaji ya viatu,hivyo tunaomba siku nyingine mje na viatu vingi zaidi”,alisema Mwita Manoti mwalimu mkuu shule ya msingi Bugogwa.
Mkurugenzi wa Taasisi ya Teknolojia ya Dar es salaam Dk. Albert Mmari akikabidhi kiatu kwa mwalimu mkuu wa shule ya msingi Sangabuye Patrodi Mpoki
Mkurugenzi wa Taasisi ya Teknolojia ya Dar es salaam Dk. Albert Mmari kiatu mwalimu mkuu wa shule ya msingi Nyafula Evodius Rwiza
Mkurugenzi wa Taasisi ya Teknolojia ya Dar es salaam Dk. Albert Mmari akimkabidhi kiatu mwalimu mkuu wa shule ya msingi Bugogwa Mwita Manoti

Wanafunzi wakiwa wamevaa viatu vipya
Wanafunzi wakivaa viatu vipya

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments