WAUZA MADINI FEKI WANASWA SIKONGE


 Na Lucas Raphael,Tabora
Mwanamke mmoja mkazi wa mkoani wa Arusha amekamatwa na Jeshi la Polisi katika stendi ya mabasi wilayani Sikonge Mkoani Tabora kwa tuhuma za kukutwa na madini feki aina ya Dhahabu  waliyokuwa wakiwauzia wananchi wa kishrikiana na dereva wake .

Akitoa taarifa kwa waandishi wa habari jana Kamanda wa Polisi Mkoani hapa ACP Richard Abwao alisema walimkamata Mariam Said, mkazi wa Arusha akiwa na dereva wake David George wakiwa na madini hayo waliyoyatumia kumtapeli mkazi wa kijiji cha Usunga wilayani humo aitwaye Edward.

Alibainisha kuwa watuhumiwa walikamatwa baada ya kumtapeli mkazi huyo kiasi cha sh 340,000 ambapo pia baada ya kukaguliwa walikutwa na kadi 5 za benki tofauti tofauti ambazo ni kadi za NMB 3, Posta 1na CRDB 1.

Vitu vinginevyo walivyokutwa navyo ni simu 4 aina ya iphone 6s plus, Tecno Spark 5 Air, Infinix hot 10 na Sam sung zinazodhaniwa kuwa za wizi.

Kamanda Abwao alibainisha kuwa madini hayo yamekamatwa kutokana na jitihada za Jeshi la Polisi kwa kushirikiana na wananchi na vyombo vya ulinzi na usalama katika kuzuia, kutanzua na kupambana na uhalifu.

Aidha aliongeza kuwa katika kukabiliana na matukio ya uhalifu, mauaji, unyang’anyi wa kutumia silaha, ujambazi na uvunjaji Mkoani humo, Jeshi hilo limeendelea kufanya oparesheni mbalimbali katika wilaya zote.

Alitaja mafanikio ya oparesheni hiyo kwa mwezi huu kuwa ni kukamatwa watu 2 Khamis Baruti na Mohamed Shaban wakazi wa Izimbili wilayani Uyui kwa kukutwa na silaha aina ya gobore isiyo na namba za usajili iliyokuwa ikitumika kwenye uwindaji haramu.

Aidha walikamata silaha 2 aina gobore zilizosalimishwa na watu wasiojulikana katika kata za Kipanga na Mole ( Usanganya) wilayani Sikonge na silaha nyingine ilisalimishwa na mkazi wa Mibono John Matuzya katika Ofisi ya Mtendaji wa Kata ya Kiloleni akidai anatii sheria bila shuruti.

Kamanda alitoa wito kwa wananchi wanazomiliki silaha kinyume na utaratibu kuendelea kuzisalimisha ndani ya kipindi hiki cha msamaha wa Waziri wa Ulinzi vinginevyo watakamatwa, aliitaka jamii kuendelea kushirikiana na Jeshi hilo kwa kutoa taarifa za vitendo vya uhalifu na wahalifu.


Mwisho.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments