BENKI YA I&M YAZINDUA TAWI JIPYA ARUSHA


Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Jphn Mongella akizindua tawi jipya la benki ya I&M lililopo Arusha.Wengine ni Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki hiyo, Baseer Mohammed pamoja na Meneja wa Wateja wa rejareja Lilian Mtali.Tawi hilo ni la kisasa zaidi na litatoa huduma kulingana na mahitaji ya wateja ikiwamo huduma ya Slect Banking kwa wateja wakubwa.
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, John Mongella akizungumza wakati wa uzinduzi wa tawi jipya la benki ya I&M lililopo Arusha. Tawi hilo ni la kisasa zaidi na litatoa huduma kulingana na mahitaji ya wateja ikiwamo huduma ya Select Banking kwa wateja wakubwa.
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, John mongella (Katikati) kwenye picha na Afisa mtendaji Mkuu wa benki ya I&M, Baseer Mohammed (Kulia), Meneja wa wateja wa rejareja wa I&M Lilian Mtali wakati wa uzinduzi wa tawi jipya la benki hiyo lililopo Arusha.


***

Arusha ,30 Novemba, 2021.

Wateja wa benki ya I&M mkoani Arusha wataondokana na adha ya kutembea umbali mrefu kufuata huduma baada ya benki hiyo kuzindua tawi jipya na la kisasa lililopo katikati ya mji.

Tawi hilo litatoa huduma mbalimbali kulingana na mahitaji ya wateja ikiwa huduma ya Select Banking ambayo ni mahususi kwa ajili ya wateja wa juu.

Tawi hilo lilizinduliwa na Mkuu wa Mkoa wa Arusha, John Mongella kwa niaba ya Waziri wa Fedha na Mipango na kushuhudiwa na viongozi mbalimbali akiwamo Mwakilishi wa Benki Kuu ya Tanzania (BoT) Emmanuel Akaro.

Akizungumza wakati wa uzinduzi, Afisa Mtendaji Mkuu wa Benki hiyo, Baseer Mohammed alisema lengo la kuhamisha tawi hilo lilikuwa ni kurahisisha upatikanaji wa huduma kwa wateja wake mkoani Arusha.

“Hatua hii ya kuhamisha ni mkakati wa kuhakikisha wateja wetu wanapata huduma kwa urahisi zaidi.Tawi hili ambalo lipo katikati ya mji, lina miundombinu ya kisasa na huduma mbalimbali kama Select Banking kwaajili ya wateja wakubwa,” alisema.

Tawi hilo limehamishwa kutoka mtaa wa Jakaranda-Falcon Building na kupelekwa mtaa wa Goliondoi jengo la Sunda Plaza.Eneo hilo la kimkakati linatarajiwa kuongeza mzunguko wa biashara mkoani humo.

Akizindua tawi hilo, Mkuu wa Mkoa wa Arusha, John. Mongella aliipongeza benki hiyo kwa hatua hiyo akisema itasaidia kuchochea shughuli za kiuchumi kwa wakazi wa Arusha pamoja na wageni ambao wengi wao ni watalii.

“Huduma za benki ni muhimu sana katika kuchochea uchumi wa Taifa;hatua hii ni ishara kwamba sekta hii iko imara na inaendelea kukua kila siku,” alisema

“Uwepo wa tawi hili ambalo ni la kisasa itasaidia kuongeza mzunguko wa biashara, kukuza shughuli za utalii pamoja kuongeza ukusanyaji wa mapato,” alisema.

Benki hiyo ina matawi nane yaliyoko Dar es Salaam, Mwanza, Kilimanjaro na Arusha na inatarajia kuendelea kupanua kwenye mikoa mingine.

Benki hiyo imekuwa mstari wa mbele kuendeleza matumizi ya teknolojia kidigitali kwa kuanzisha bidhaa na huduma kama WhatsApp Banking,Kamilisha na Kadi VISA ya Malipo ya kabla.

Kumekuwa na ongezeko la mali za benki kwa asilimia 11.2% kwa mwaka ikifanikiwa kupata Tsh567 bilioni kwa mwaka ulioisha Oktoba 2021.Kwa mwaka huo, kulikuwa na ongezeko la asilimia 12.3 kwenye mikopo (Net Advances) na amana za wateja kwa asilimia 19.


Aliipongeza benki kwa kuanzisha huduma ya Select Banking ambayo ni maalumu kwa wateja wakubwa na kwamba itasaidia kukuza shughuli za kiuchumi ikizingatiwa kuwa mkoa huo umetawaliwa na shughuli zenye mzunguko mkubwa ikiwa utalii na uchimbaji wa madini.

Meneja wa wateja wa rejareja wa I&M, Lilian Mtali alisema benki hiyo imejikita zaidi katika kutoa huduma za kidigitali na kuwa moja ya benki chache zinazotoa huduma kwa njia ya WhatsApp kupitia huduma yake ya Rafiki ChatBanking.

“Kwenye hili tawi pia tumezindua huduma ya kubadilisha fedha ambayo itapatikana kwa masaa mengi zaidi ili kuwapa wateja nafasi ya kupata huduma hii muda wowote.Pia, tuna huduma ya kuhifadhi nyaraka na vitu vya thamani ambayo itamsaidia mteja kutunza vitu vyake kwa usalama zaidi,” alisema.

Download/Pakua/Install App ya Malunde 1 blog Google Playstore Bofya Hapa

Je, unayo taarifa ya kusisimua ambayo ungependa tuichapishe? Tafadhali, wasiliana nasi kupitia malundekadama@yahoo.com au WhatsaApp: + 255 757 478 553 au 0625 918 527

0/Post a Comment/Comments